2014-08-18 09:06:37

Fadhila ya ukweli!


Mpendwa msikilizaji wa kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo! Karibu kwa mara nyingine tena katika kipindi chetu pendevu. Kwa sasa tunazitembelea fadhila mbalimbali zenye kutusaidia katika maisha yetu ya kila siku. RealAudioMP3

Tunajifunza fadhila hizi ili sisi wenyewe tujiunde hivi tuwe watu tunaopokeleka na kufikika katika maisha yetu ya kila siku. Ni imani yetu kwamba, ni jukumu la kila mmoja kuchangia katika hali njema ya jumuia tunamoishi. Kwa lile kanisa la nyumbani ambalo kimsingi ni shule ya maadili na fadhila, tusikose kuwafundisha watoto wetu fadhila hizi. Huko ndiko wanakoanza kuundwa katika utu wema.

Kwa siku ya leo tutazame ukweli kama fadhila. Ukweli ni nini? Ni uwiano kati ya kinachosemwa, hali halisi na hukumu ya akili. Kwa mfano kama kinachosemwa ni mtu, katika uhalisia awe ni mtu na akili ihukumu kuwa kweli huyu ni mtu. Tunapotazama ukweli kama fadhila kwa siku hii ya leo, tunataka tujinidhamishe katika kupenda kusema ukweli daima.

Nyakati zetu hizi, kumezuka na kukua sana utamaduni wa kusema uwongo, yaani kuficha ukweli. Watu tunasema uwongo mwingi sana hata usio na tija yoyote. Kutokana na kutokuwa wakweli mdomoni mara nyingi, tumekwisha kuziathiri na akili zetu nazo, hazipendi tena kufikiri ukweli. Kuna wanaosema kwamba matumizi ya simu za mkononi nyakati zetu yamechangia sana kujengeka kwa tabia ya uongo. Ukweli wa hilo sina uhakika. Simu huwa haisemi uwongo, ni mtumiaji ndiyo husema uongo.

Mtume Paulo anatuonya akisema “basi uvueni uwongo, kila mmoja anapaswa kumwambia mwenzake ukweli, maana kila mmoja wetu ni kiungo cha mwili wa Kristo” (Ef. 4:25). Maandiko matakatifu yanatuasa daima tuseme ukweli, uwongo ni tabia ya kishetani. Shetani ndiyo baba wa uongo, na vitoto vyake vyote vina tabia ya baba yao. Maanake uongo unatushetanisha, tunafanana na shetani. Yoshua bin Sira anasema “kataa kabisa kusema uongo, maana uongo hauleti jema lolote (7:13), maana kama vile aibu imjiavyo mwizi ndivyo hukumu kali itakavyompata mdanganyifu” (5:14).

Tena Yoshua Bin Sira anaendelea kutuonya juu ya ubaya wa uongo akisema “uongo ni doa baya sana kwa mtu; uko daima mdomoni mwa mpumbavu. Afadhali mwizi kuliko mwenye tabia ya uongo. Lakini wote wawili wataangamia. Tabia ya kusema uongo huleta fedheha, nayo itabaki daima na mwenye kusema uongo” (YbS.20:24-26).

Kama kawaida yetu, rai tunaipeleka katika Kanisa la nyumbani, yaani familia. Wazazi na wote wenye dhamana ya malezi, tuwafundishe na tuwajenge watoto wetu katika roho ya kupenda kusema ukweli. Ni bahati mbaya pale ambapo watoto wetu hujifunza kusema uongo kutoka kwetu sisi watu wazima. Familia ya watu waongo huwa haifilisiki fujo. Baba mwongo, daima anamdanganya mama, mama naye mwongo daima anamdanganya baba, watoto nao lazima watafundishwa kusema uongo ili kulinda uovu wa wazazi. Wazazi waliozoea kudanganyana, lazima watawafundisha watoto kusema uwongo. Ukweli ukitoweka, kila kitu kinakuwa na wasiwasi.

Walimu pia huko mashuleni, wawanidhamishe watoto kusema ukweli daima. Pasipo kujenga akili katika kuheshimu na kupenda kusema ukweli, tunajenga jamii ya waongo. Na uongo ukitawala katika kila kona ya utendaji, hapo ufanisi hautapatika na hatutafikia malengo, kwa vile waongo na wasingiziaji wenye kujitetea kwingi kwa sababu za uongo. Kukosekana kwa ukweli wa maneno na ukweli wa mambo, husababisha mateso katika jamii.

Mtu asiyependa ukweli, mwenye kububujika maneno ya uwongo daima, huwa anaharibu utulivu wa watu waishio kwa amani. Mzaburi anataja ukweli kama mmoja ya sifa za mtu anayestahili kukaa katika hema ya Bwana. Anauliza na kujibu “Bwana ni nani atakaye kaa hemani mwako?...ni mtu atendaye daima yaliyo mema, asemaye ukweli kutoka moyoni” (rej. Zab. 15:1-2).

Mpendwa msikilizaji, na tujinidhamishe katika kusema ukweli. Uongo unachukiza sana. Na mtu akizoea kusema uongo, atausema tu kila wakati hata bila sababu. Ukweli humpa mtu heshima, uongo humletea mtu fedheha na dharau. Ukweli hutupatia uhuru na usalama. Na Kristo alisema “ukweli utawapeni uhuru”. Mpendwa msikilizaji, fanya kama zoezi la kiroho, anza polepole kujizoeza kusema ukweli. Siku nzima ipite bila kusema uwongo, kisha wiki zima, kisha mwezi mzima, na baadaye itakuwa fadhila ya kudumu, kuenenda bila kusema uwongo. Tunakutakia zoezi jema!

Kutoka katika Studio za Radio Vaticani, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.