Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili asubuhi tarehe 17 Agosti 2014 amekutana na kuzungumza
na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Asia, FABC, kwenye madhabahu
ya Haemi, ambayo kimsingi ni kumbu kumbu ya Mashahidi waliojitosa bila ya kujibakiza
kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Kuna watakatifu wengi ndani ya Kanisa ambao majina
yao hajaandikwa kwenye vitabu vya watakatifu, lakini ni kielelezo cha utakatifu wa
Kanisa.
Baba Mtakatifu katika hotuba yake amekazia zaidi dhamana na utume
wa Kanisa Barani Asia, sehemu ambayo ina utajiri mkubwa wa tamaduni na mapokeo; mahali
ambapo Kanisa linachangamotishwa kutoa ushuhuda wa Injili kwa njia ya majadiliano
yanayojikita katika ukweli na uwazi kwa wote. Katika mchakato wa majadiliano ya kidini,
Wakristo watambue utambulisho wao na kuutolea ushuhuda makini katika misingi ya ukweli
na uwazi, ili yaweze kuzaa matunda yanayokusudiwa.
Wakristo watambue mambo
makuu ambayo Mwenyezi Mungu amewatendea katika hija ya maisha yao na kwamba, kuna
mambo ambayo Mwenyezi Mungu anayataka kutoka kwa Wakristo. Ili majadiliano haya yaweze
kuwa na mwelekeo wa pande mbili, lazima Wakristo wafungue akili na mioyo, ili kuwakubali
na kuwapokea watu wengine pamoja na tamaduni zao. Hapa Baba Mtakatifu anakazia mambo
makuu mawili, yaani ushuhuda na majadiliano na kwamba, kuna mambo makuu matatu ambayo
yanapaswa kuangaliwa na kuepukwa katika hali ya ukomavu.
Kwanza kabisa anasema
Baba Mtakatifu ni mawazo mepesi mepesi yanayowasukuma wengi katika hali ya kuchanganyikiwa
na kukata tamaa. Hiki ni kishawishi kikubwa ambacho kinagusa pia Jumuiya za Kikristo,
ambazo zinapaswa kutambua kwamba, Yesu Kristo ndiye msingi wa maisha yao. Yeye ni
alfa na omega, nyakati zote ni zake. Mawazo mepesi mepesi si tu kwamba, yanajitokeza
kama dhana bali pia yanamwilishwa katika matendo bila ya wengi kufahamu na hivyo kudhohofisha
utambulisho wa aina yoyote ile!
Baba Mtakatifu anasema, jambo la pili linalohatarisha
msingi wa utambulisho wa Wakristo ni kufanya mambo kwa juu juu tu bila kuzamisha mizizi
hasa katika shughuli za kichungaji, kwani mambo mengi yanafanyika kama mtindo wa maisha,
unaovamia na kutoweka mara. Hii ni mikakati ya kichungaji ambayo inavutia machoni
pa pa watu kutokana na nadharia zake hasa miongoni mwa vijana.
Lakini, Baba
Mtakatifu anasema, vijana wanahitaji katekesi makini na viongozi thabiti katika maisha
ya kiroho; kwa kukita mizizi kwa Yesu na katika kweli, vinginevyo maisha ya fadhila
yatageuka kuwa kama mchezo wa kuigiza, majadiliano ya dhati yatageuka kuwa ni "mchapo"
kwa kukubaliana au kutokubaliana.
Baba Mtakatifu anaendelea kusema kwamba,
kishawishi cha tatu ni usalama unaojificha katika majibu mepesi mepesi, sentesi zilizokwisha
kupikwa, sheria na kanuni. Imani kimsingi haijitafuti yenyewe bali ina tabia ya kutoka
nje. Ni zawadi inayojieleza kwa watu ili waweze kuifahamu, kiasi hata cha kuweza kuimwilisha
na kuitolea ushuhuda katika matendo; imani inaibua utume.
Utambulisho wa Kikristo
unajipambanua kwa kuwa na dhamana ya kumwabudu Mwenyezi Mungu na kuwapenda jirani;
kujisadaka kwa ajili ya huduma, kama kielelezo cha ushuhuda wa kile wanachoamini na
yule ambaye wamemwekea matumaini yao. Imani hai kwa Kristo ndio msingi madhubuti wa
utambulisho wao wa kina unaozaa matunda yanayokusudiwa. Ni imani inayozaliwa na kurutubishwa
na neema ya majadiliano na Kristo katika mwanga wa Roho Mtakatifu, kiasi cha kuzaa
haki, wema na amani.
Baba Mtakatifu Francisko kwa namna ya pekee, anawataka
Maaskofu Katoliki Barani Asia kuhakikisha kwamba, utambulisho wao wa Kikristo unajitokeza
kwa nguvu kabisa katika proramu za katekesi, mikakati ya kichungaji miongoni mwa vijana
na huduma makini kwa maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Utambulisho
huu ujioneshe katika mchakato wa kuwahamasisha vijana kujiunga na maisha ya Kipadre
na Kitawa.
Mwishoni mwa hotuba yake kwa Maaskofu kutoka Barani Asia, Baba Mtakatifu
anasema, kuna haja ya kuwa na utambulisho wa Kikristo uliowazi kabisa, kwani majadiliano
ya kweli yanahitaji uwezo wa mtu kuguswa na mahangaiko ya wengine. Kanisa lioneshe
uwezo wa kusikiliza si tu maneno yanayozungumzwa na watu, bali liguswe pia uzoefu,
matumaini, matarajio, matatizo na mambo msingi ambayo wanayapatia kipaumbele cha pekee.
Tabia
hii ya kuguswa na mahangaiko ya wengine iwe ni matunda ya mwelekeo wa maisha ya kiroho
na uzoefu wa mtu binafsi unaowawezesha waamini kuwathamini wengine kama ndugu zao,
ili kuwasilikiza kwa makini, licha ya maneno na matendo yao, bali kile ambacho wanapenda
kuwashirikisha kutoka katika undani wa mioyo yao. Mwelekeo huu wa ukweli na uwazi
kwa uwe ni mwongozo hususan Barani Asia ambako Vatican haijafanikiwa kuwa na uhusiano
mkalimifu, ili kukuza na kuendeleza majadiliano si tu ya kisiasa bali majadiliano
ya kidugu kwa ajili ya mafao ya wengi.
Mara baada ya hotuba yake, Baba Mtakatifu
Francisko na msafara wake pamoja na Maaskofu kutoka katika Shirikisho la Mabaraza
ya Maaskofu Katoliki Barani Asia walipata chakula cha mchana.