2014-08-17 10:59:19

Msifanyie mzaha ugonjwa wa Ebola, toeni ushirikiano!


Kardinali Thèodore Adrien Sarr, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dakar, Senegal anawataka wananchi pamoja na viongozi wa Serikali nchini humo kuwa makini katika kupambana na ugonjwa wa Ebola ambao kwa sasa umekuwa ni tishio kubwa la maisha na usalama wa wananchi kutoka Afrika Magharibi. Ugonjwa huu unaendelea kusababisha mateso na mahangaiko kwa watu wengi, kiasi kwamba, watu wengi wamechanganyikiwa kutokana na madhara yanayosabishwa na ugonjwa huu.

Kardinali Sarr amewataka wananchi kutambua ukumbwa wa tatizo hili na kwamba, watu wengi wameguswa na madhara yake, kumbe hakuna sababu ya watu kufanya mzaha kuhusu kujikinga na kuchukua hatua madhubuti dhidi ya kuenea kwa ugonjwa huu ambao umetangazwa kuwa ni janga la kimataifa. Wananchi waoneshe ushirikiano kwa Wizara ya afya na Serikali pale wanapotambua wagonjwa walioambukizwa virusi hivi katika maeneo yao, ili hatua madhubuti ziweze kuchakuliwa haraka.

Kardinali Thèodore Adrien Sarr ameyasema haya wakati wa maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni mwili na roho, kwenye madhabahu ya Popenguine, Jimbo kuu la Dakar, Senegal. Amewakumbuka watu wanaoendelea kuteseka kutokana na vita nchini Syria na wale wanaodhulumiwa na kunyanyaswa kutokana na imani yao Kaskazini mwa Iraq.

Kardinali Sarr amewataka viongozi wa kidini nchini Senegal kujibidisha katika kufunda dhamiri nyofu, ili wawe waweze kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu kwa kujielekeza zaidi katika misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati. Tofauti mbali mbali zinazojitokeza katika maisha ya watu ni utajiri mkubwa na kamwe kisiwe ni chanzo cha vita na maafa kwa watu wasiokuwa na hataia. Hapa kuna haja ya kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya uhai dhidi ya utamaduni wa kifo, ili watu waishi kwa amani na utulivu wakifurahia maisha yao!







All the contents on this site are copyrighted ©.