2014-08-17 10:41:59

Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo na Familia ni chanda na pete!


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA linaendelea kukazia kuhusu Uinjilishaji Mpya kama fursa inayowawezesha waamini kujikita katika wongofu wa ndani na ushuhuda wa imani ya Kanisa Katoliki kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa tunu msingi za maisha ya kifamilia na umuhimu wa Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo. RealAudioMP3

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Padre Raymond Saba, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania anasema kwamba, familia ni nguzo msingi katika kurithisha imani, utu na maadili mema. Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo ni sehemu ya pili ambayo inapaswa kuwa ni matunda ya familia thabiti za Kikristo, ili kuimarisha msingi wa Kanisa mahalia.

AMECEA imeendelea kukazia uimarishaji wa mikakati ya kichungaji kwa ajili ya Familia pamoja na Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo. Ujenzi wa Kanisa mahalia hauna budi kuanza katika familia na baadaye kuimarishwa katika Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo kwani hapa ni mahali ambapo Wakristo wanakutana kusali, kutafakari na kumwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha yao.

Ni mahali pa kuimarisha katika imani, matumaini na mapendo, tayari kumwilisha imani kwa Kristo na Kanisa lake katika matendo. Jumuiya ndogo ndogo ni shule ya ukarimu, huruma na mapendo ni mahali pa kuimarishana katika maisha ya Kisakramenti. Padre Raymond Saba anasema Familia na Jumuiya ndogo ndogo zilizokomaa ni kielelezo cha uhai wa Kanisa mahalia.








All the contents on this site are copyrighted ©.