2014-08-17 10:34:47

Injili ya Familia ya Kikristo!


Askofu Gervas Rozario wa Jimbo Katoliki la Rajshahi, huko Bangaladesh anasema kwamba, matatizo na changamoto mbali mbali zinazoikumba familia ni sehemu ya maisha na utume wa Kanisa kwani Kanisa linatambua kwamba, Familia ni chombo muhimu sana katika kurithisha imani, maadili na utu wema ndani ya Jamii na kwamba, ni nguzo msingi ya maisha ya kijamii. RealAudioMP3

Katika barua yake yake ya kichungaji inayoongozwa na kauli mbiu “Utangazaji wa Injili ya Familia ya Kikristo” anafafanua kwamba, Familia ni muhimu sana katika maisha, ustawi na maendeleo ya jamii husika kama ilivyo pia hata kwa Mama Kanisa. Kumbe, Kanisa litaendelea kuwekeza katika tunu msingi za maisha ya ndoa na familia kwa kutambua kwamba, kila familia ya Kikristo ni Kanisa dogo la nyumbani, linalowajibika kuwa ni moja, takatifu, katoliki na la mitume, tayari kuwatangazia wengine Injili ya Furaha kwa njia ya ushuhuda wa maisha.

Katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, familia inakumbana na umaskini wa hali na kipato, ulevi wa kupindukia, kinzani za kifamilia, utamaduni wa kifo unaokumbatiwa na sera za utoaji mimba na kifo laini; ndoa za chapu chapu pasi na msingi kamili wa upendo! Kukua na kuongezeka kwa familia tenge ambazo nyingi zinahudumiwa na wanawake peke yao kutokana na wazazi wa kiume kwenda kutafuta riziki mbali na familia zao pamoja na ukosefu wa mbinu makini za mawasiliano kati ya wanandoa na matokeo yake ni wanandoa kukosa amani na furaha ya ndoa.

Injili ya Familia ya Kikristo inapenda kukuza na kuimarisha tunu bora za maisha ya ndoa na familia kwa kuhakikisha kwamba, familia zinatekeleza wajibu wake wa malezi kwa watoto wao. Hapa Kanisa linapenda kujenga na kukuza sanaa ya mawasiliano kati ya wanandoa, ili wanapowasiliana basi iwe ni fursa ya kushirikishana upendo unaojielekeza zaidi katika umoja, majadiliano, msamaha na haki.

Mihimi ya Injili, yaani Mapadre, Watawa na Makatekista wanahamasishwa kutembelea familia, ili kuzisaidia katika kutambua wajibu wake katika maisha na utume wa Kanisa sanjari na kuendeleza majiundo makini kwa wanandoa watarajiwa ili waweze kufahamiana, kupendana na kuheshimiana. Kwa wale wambao wanaishi tayari katika maisha ya ndoa na familia wanapaswa kupewa Katekesi endelevu, ili kung’amua changamoto zinazoweza kujitokeza katika maisha yao, ili kuweza kuzikabili kwa busara, upendo na ujasiri.
Vijana wa kizazi kipya waelimishwe ili kutambua umuhimu wa maisha ya ndoa na familia, ili wawe tayari kufanya maamuzi magumu katika maisha yao kwa kuchagua kufunga ndoa ya Kikristo na kufuata masharti yake, yaani hadi pale kifo kitakapowatenganisha. Yataka moyo kweli kweli kufunga ndoa ya Kikristo. Vijana wafahamiane kwanza na wakubaliane kwa kusukumwa na upendo thabiti na wala si makando kando yake, kama vile pochi! Waswahli wanasema, hapendwi mtu, ila pochi, lakini kumbe haya ni mambo mpito!

Askofu Gervas Rozario anasema kuna baadhi ya Wakristo ambao wanaendelea kuishi katika uchumba sugu, hawa pia ni walengwa katika mikakati ya kichungaji, ili kurekebisha hali yao tayari kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa na wala wasiwe ni watazamaji hasa wakati wa kushiriki Sakramenti za Kanisa.








All the contents on this site are copyrighted ©.