2014-08-15 09:57:53

Kardinali Filoni aomba msaada wa Kimataifa


Kardinali Fernando Filoni ,aliyetumwa na Papa Francisco kwenda Iraki, kwa lengo la kuwa karibu na kushikamana na wateswa wa madhulumu yanayofanywa Iraki na makundi ya Waislamu wapiganaji “wanajihad”, Jumatano alitembelea eneo la Erbil ya Kurdistani ya Iraki. Kardinali kwa upendo na huruma kubwa alisalimia na kukumbatiana na makundi ya watu walioacha nyumba zao wakiwa mikono mitupu kutoka eneo la ukanda wa Ninive.

Katika mahojiano na Sergio Centofanti wa Redio Vatican ,juu ya hali halisi ilivyo baada ya kutembelea kambi kadhaa za wakimbizi hao, alisema, jambo la kwanza, amesalimiana n akukumbatiana na mamia ya watu waliokusanyika kila mahali katika eneo hilo , si tu katika bustani za jengo la Askofu, lakini pia waliopata mahali pa kuweka kichwa, ndani ya jengo la Kanisa na shuleni pia. Kuna mamia kwa mamia ya watu waliokusanyika hapo. Na hivyo, kazi ya kwanza kwa Kanisa, imekuwa kuwapokea na kuwafanikisha kuishi watu hawa walio katika hali ngumu na hatarishi. Kwa bahati wakati huu si kipindi cha baridi, ingawa kuna joto kali lakini bado ni ahueni kuliko kuwa nje kwenye baridi kali. Na ndani ya majengo walau kuna kiyoyozi na hasa sehemu walikowekwa watoto. Na nyakati za usiku watu wanaweza kulala nje ambako hewa ni mwanana. Na kwamba mipangilio ya kuwaweka watu hao katika eneo ndogo inakwenda vizuri, kuna wema na fadhila nyingi.

Aidha Kardinali Filoni, akiitazama hali ya kisiasa, baada ya kukutana na kuzungumzana uongozi, akiwemo Rais wa Mkoa wa Kurdistan, Rais Mas’ud Barzani , ameona kwamba, wako tayari kutoa msaada na wameonyesha kujali ombi la Baba Mtakatifu la kupokea wakimbizi hawa, na kuhakikisha, wanapata mahitaji msingi kimaisha. Na si kimaisha tu lakini hata katika mambo mengine muhimu kwa mfano jinsi ya kusaidia wanafunzi waliokatisha masomo yao , wengine wakiwa katika vipindi cha mitihani, upatikanaji wa huduma ya tiba na dawa na uwepo wa utaratibu mzuri wa kusimamia na kugawa misaada ili wote waweze kupata mahitaji yao msingi. Kardinali anaeleza kwamba , baadhi ya kambi wameamua kuwa na jiko moja na wanajenga mabafu na vyoo vya muda, na pia wanajaribu kusaidia baadhi ya familia ziweze kupangisha nyumba.

Na kwamba, aliwasilisha msaada uliotolewa na Papa kwa Askofu mahalia ambaye ametoa kwa wahitaji kupitia taratibu zilizopo, na kwamba watu wameonyesha shukurani kubwa kwa Papa si kwa ajili tu ya msaada wa kihali lakini zaidi ya yote, kwa kupaza sauti yake kukemea madhulumu yanayowaweka watu katika hali hizi ngumu . Katika eneo hili la Arbil, kuna wakimbizi karibia 160 elfu kati yao, wakiwemo Wakristo na waamini wa madhehebu mengine madogomadogo .

Katika mahojiano hayo, Kardinali Filoni, aliieleza hali halisi ya usalama katika eneo hili kwmba bado ni tete. Na inaona bado kuna matatizo ya kuweza kutetea usalama wa nchi na watu wake. Na hivyo kwa hilo , Kardinali ametoa wito kwa jumuiya ya kimataifa, kutoa msaada wake si wa vitu tu lakini hasa msaada wa kisiasa na kijeshi. Utawala unaona kuwa ni jambo nyeti sana kuomba msaada kwa jumuiya ya kimataifa. Na pia kwa wakati huu serikali ya Kurdistan haioni kama ni jambo lazima sana kufanya hivyo kwa wakati huu.

Kardinali Filoni anasema, pamoja na mahitaji yote hayo ya kihali, pia kuna kiu ya kiroho na kisaikolojia kwa watu wengi. Na hivyo anatumaini kwa msaada wa kihali unaotolewa kwa watu wote katika siku hizi uwezeshe pia kutoa utulivu wa kiroho na kisaikolojia, wakati watu hao watakapoweza kurejea makwao.








All the contents on this site are copyrighted ©.