2014-08-14 09:20:02

Papa Francisko amewasili tayari Korea ya Kusini!


Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa ndege wa kimataifa mjini Seoul amepokelewa na viongozi wa Kanisa na Serikali ya Korea ya Kusini, itifaki ikiwa imezingatiwa. Vikosi vya ulinzi na usalama vilipiga mizinga ishirini na moja kama alama ya kumkaribisha Baba Mtakatifu nchini Korea.

Baba Mtakatifu siku ya Alhamisi asubuhi tarehe 14 Agosti 2014 kwa saa za Korea ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na sehemu kubwa ya mahubiri yake yamegusia kwa muhtasari hija yake ya kitume nchini Korea ya Kusini.

Baba Mtakatifu Francisko kabla ya kuondoka kuelekea nchini Korea ya Kusini kwa ajili ya hija yake ya kitume, Jumatano asubuhi, tarehe 13 Agosti 2014 alikwenda kusali kwa faragha kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu lililoko mjini Roma, ili kuiweka hija yake ya kitume nchini Korea, chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria. Akiwa Kanisa hapo, Baba Mtakatifu aliweka shada la maua kwa Sanamu ya Bikira Maria.

Akiwa njiani kuelekea Nchini Korea ya Kusini, Baba Mtakatifu alipata nafasi ya kuzungumza na waandishi wa habari ambao wako katika msafara wake. Kwa pamoja wamesali na kumwombea mwandishi wa habari Simone Camilli kutoka Italia aliyeuwawa kwenye Ukanda wa Ghaza wakati akitekeleza kazi yake kama mpiga. Baba Mtakatifu anasema, haya ni madhara ya vita.

Baba Mtakatifu amewashukuru waandishi wa habari kwa huduma yao kwa kutambua kwamba, wakati wa hija hii ya kitume wanayo kazi kubwa ili kuhakikisha kwamba, ulimwengu unahabarishwa kile kinachoendelea katika hija yake ya kitume nchini Korea. Wakati wa kipindi cha kiangazi, kazi inakuwa na ugumu wake kutokana na uwepo wa joto kali.

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu amewahimiza waandishi wa habari kuwa ni wajumbe wa amani, kwani kwa sasa kuna majanga mengi yanayoendelea kujitokeza sehemu mbali mbali za dunia, hali ambayo inatisha.







All the contents on this site are copyrighted ©.