2014-08-14 15:38:08

Mwaka wa Familia, Jimbo kuu la Dar es Salaam!


"Wakati Yesu alipokaribia Yeriko, kulikuwa na mtu mmoja kipofu ameketi njiani akiomba. Aliposikia umati wa watu ukipita aliuliza, kuna nini? Wakamwambia, Yesu wa Nazareti anapita. Naye akapaza sauti akisema, Yesu, Mwana wa Daudi, nihurumie! Wale watu waliotangulia wakamkemea wakamwambia anyamaze; lakini yeye akazidi kupaza sauti: Mwana wa Daudi, nihurumie! Yesu alisimama, akaamuru wamlete mbele yake.

Yule kipofu alipofika karibu, Yesu akamuuliza, unataka nikufanyie nini? Naye akamjibu, Bwana, naomba nipate kuona. Yesu akamwambia, Ona! Imani yako imekuponya. Na mara huyo kipofu akapata kuona, akamfuata Yesu akimtukuza Mungu. Watu wote walipoona hayo, wakamsifu Mungu (Lk 18:35-43).

Mwinjili Luka anatusimulia jinsi huyu kipofu alivyoichukia hali yake ya upofu na hivyo kutafuta msaada. Huenda alishahangaika sana kujitibia lakini ikashindikana, na ndipo akalipeleka tatizo lake la upofu kwa Yesu naye anamtoa upofu wake.

Wapendwa sisi wote ni vipofu wa mambo mengi. Bahati mbaya hatujaufahamu upofu wetu, na hivyo hautukerwi na hali hiyo hata kutusababisha kutafuta dawa ya upofu wetu. Mara ngapi tunapata muda wa kukesha bar, kuhudhuria vikao vya harusi, kutazama TV kwa muda mrefu, lakini tukakosa muda wa kusali binafsi na katika familia. Au, kushindwa kwenda kanisani, kwenye jumuiya ndogondogo na kufuatilia mafundisho ya Mungu kutokana na kukosa muda au kuchoka? Huo ni upofu!

Mara ngapi tunatumia fedha nyingi kwa kununua vitabu vya hadithi, kufurahia kusoma magazeti ya udaku, kusoma vitabu vya hadithi, lkn tukakosa pesa ya kununuli Biblia (ambapo ungenunua mara moja kwa miaka mingi), kushindwa kusoma Biblia na kusimuliana mafundisho ya Mungu? Huo ni upofu!

Ni mara ngapi tunachangia fedha nyingi katika maharusi na sherehe mbalimbali (mtu anakuwa na kadi za kuchangia harusi, kicheni pati n.k. hata nne kwa mwezi), lakini hatuwezi kuchangia elimu ya watoto wahitaji na kuwa makanisani michango mingi hadi inaboa? Huo ni upofu!

Ni mara ngapi tunakumbuka kununua vocha za simu zetu, kulipa bili za umeme, kulilia ving'amuzi km Dstv, Startime Azam n.k, lakini tunajisahaulisha kulipa zaka kamili ili Mungu atuongezee kipato chetu na kutuepusha na majanga? Huo ni upofu!
Ni mara ngapi tunapenda kuwasaidia "wasio na shida", kuwafurahisha marafiki kwa 'kuwazungushia' raundi za vinywaji, kuwahudumia vimada, lkn wazee wetu, watoto wetu na familia zetu zinateseka kwa kukosa mahitaji ya lazima ya kila siku? Huo ni upofu!

Ni mara ngapi tunapenda kuomba msamaha, kuwasamehe marafiki zetu na watu wengine, lakini tunashindwa kutoa msamaha kwa wenza wetu wa ndoa, kwa watoto wetu, familia zetu hata tunashindwa kuongea nao wakati tunaishi nao nyumba moja? Huo nao ni upofu!

Sisi wote ni vipofu, wapendwa, tunaohitaji uponyaji wa Mungu. Tumuombe Mungu atuponye upofu wa uelewa wetu ili tubadilike kutoka kutenda na kuyapenda yale yasiyo na faida na thamani halisi ya maisha yetu na kuanza kuona mwanga wa kweli katika kutekeleza wajibu zetu kwa Mungu, kwa kanisa, kwa wazazi wetu, wenza wetu, watoto wetu, kwa wenye mahitaji muhimu katika jamii zetu na kutenga muda kwa ajili ya maandiko Matakatifu, sala za familia, misa Takatifu na maongezi ya kiipendo katika familia.

Tumsifu Yesu Kristu!

Imetayarishwa na Antipasi Shinyambala.








All the contents on this site are copyrighted ©.