2014-08-13 12:07:05

Watoto wanastahili kulindwa na kuheshimiwa!


Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI amekipongeza chama cha kitume cha Meter kwa kujisadaka kwa ajili ya: ulinzi, ustawi na maendeleo ya watoto, kwani watoto ni tumaini la Kanisa na Jamii katika ujumla wake na kwamba, watoto ni matumaini ya Kanisa la Kristo.

Ni kutokana na kuguswa na mahangaiko ya watoto ndiyo maana viongozi wa Kanisa wameendelea kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Chama hiki cha kitume kwa ajili ya kuwalinda na kuwatetea watoto, tangu wakati wa uongozi wa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI hadi wakati huu anapoongoza Papa Francisko!

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI anamshukuru na kumpongeza Padre Fortnato Di Noto kwa kuchapisha kitabu ambacho kimemvutia sana Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI. Hiki ni kitabu ambacho kina mchango wa Makardinali 8 na Maaskofu 70 waliotuma ujumbe wao katika kipindi cha miaka kumi iliyopita katika maadhimisho ya Siku dhidi ya nyanyaso za kijinsia kwa watoto wadogo.

Kitabu hiki, kadiri ya barua iliyochapishwa na Sekretarieti ya Vatican kinaonesha urafiki mkubwa kati ya Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI na Padre Fortunato, kuhusu mwelekeo wa elimu nchini Italia. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI anaendelea kumtia shime, kusonga mbele katika mchakato wa majiundo makini na elimu nchini Italia.







All the contents on this site are copyrighted ©.