2014-08-11 09:23:41

Matumaini ya Kanisa Katoliki nchini Korea ya Kusini


Baraza la Maaskofu Katoliki Korea kwa namna ya pekee kabisa linapenda kumshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kuonesha moyo wa ujasiri na utashi wa kutembelea Korea, cheche ya matumaini katika mchakato wa upatanisho wa kitaifa kati ya Korea ya Kusini na Korea ya Kaskazini. Ni hija inayopania kuwaimarisha ndugu zake katika imani. Ni maneno ya Askofu Peter U-ill Kang, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Korea katika mahojiano maaluma na Shirika la Habari la UCANEWS.

Korea ilijikuta inagawanyika na kuwa ni nchi mbili tofauti kunako mwaka 1945, lakini bado ni watu wanaozungumza lugha moja wakiwa wameshikamana na utamaduni wao na kwamba, dalili zinaonesha kuwa utengano huu hautakuwa wa muda mrefu, kwani alama za nyakati zinaonesha kwamba, watu wanataka umoja na mshikamano wa kitaifa. Mabadiliko msingi hayana budi kuchomoza kutoka ndani ya nchi husika na hadi sasa kuna cheche za mabadiliko zinazoendelea kujitokeza siku hadi siku, hasa Korea ya Kaskazini.

Wananchi wengi wa Korea ya Kaskazini wanakabiliwa na hali ngumu ya maisha kiasi kwamba, uvumilivu wao kwa sasa unaonekana kufikia ukomo. Baa la njaa kati ya watu ni chachu ya mapinduzi ya kisiasa na kijamii, ili kujikita katika mchakato wa kukuza na kudumisha haki ya kweli na demokrasia kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi.

Askofu Peter anasema, hata ndani ya Kanisa lenyewe kuna mpasuko unaojionesha kwani kuna baadhi ya Makleri wanaounga mkono Serikali na wengine wako kinyume cha utawala wa mabavu, hapa Kanisa linajikutalikiwa njia panda katika utekelezaji wa maisha na utume wake katika jamii. Mpasuko huu hauna uhusiano wowote na masuala ya Mafundisho tanzu ya Kanisa.

Ukosefu wa haki jamii ni kati ya changamoto zinazowakabili vijana wengi Korea ya Kusini, Kanisa kwa kujikita katika Mafundisho Jamii linapenda kuwapatia vijana matumaini kwa leo na kesho iliyo bora zaidi, lakini hili ni jambo linalohitaji muda na rasilimali nyingi.








All the contents on this site are copyrighted ©.