2014-08-09 11:06:23

Kanisa linapenda kukazia majadiliano yanayojikita katika ukweli, uwazi na heshima!


Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican anasema Kanisa Katoliki nchini China liko hai na linazidi kuchapa kazi, kwa kuendelea kuwa aminifu kwa Injili ya Kristo, licha ya magumu na changamoto mbali mbali linalokabiliana nazo.

Kardinali Parolin katika mahojiano maalum na Jarida la "Famiglia Cristiana" linalochapishwa nchini Italia anasema, Vatican inapenda kukazia majadiliano yanayojikita katika: ukweli, uwazi na heshima na viongozi wa Serikali ili kupata muafaka wa changamoto na vikwazo vinavyopelekea waamini wa Kanisa Katoliki kunyimwa uhuru wa kuabudu. Lengo la majadiliano haya ni kuhakikisha kwamba, kunakuwepo na mazingira mazuri ya uhuru wa kidini.

Kardinali Parolin akizungumzia hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Korea ya kusini inayoanza rasmi tarehe 13 hadi tarehe 18 Agosti 2014, ili kushiriki katika maadhimisho ya Siku ya Sita ya Vijana Barani Asia, inayoongozwa na kauli mbiu "Ondoka, uangaze, kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa Bwana umekuzukia" anasema kwamba, utafiti uliofanywa hivi karibuni nchini Korea ya Kusini unaonesha kwamba, Kanisa Katoliki linaendelea kutoa mchango mkubwa katika maisha na maendeleo ya watu: kiroho na kimwili.

Baba Mtakatifu anakwenda nchini Korea kama mjumbe wa haki, amani na upatanisho, kwa kutoa changamoto kwa Korea zote mbili kuweka tofauti zao za kisiasa zilizopelekea chuki na uhasama kwa kuanza kujikita katika mchakato wa upatanisho wa kitaifa, ili kujenga umoja na mshikamano kati ya wananchi wa Korea hizi mbili.

Ni matumaini ya Kardinali Pietro Parolin kwamba, ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko utaweza kukuta mioyo na akili ambazo zitaupokea na kuufanyia kazi, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Korea zote mbili. Korea ya Kusini imebahatika kuwa ni nchi ya kwanza Barani Asia kuonesha ukarimu kwa kumpokea Baba Mtakatifu Francisko, hapa inaonesha jinsi ambavyo Baba Mtakatifu anajali na kuguswa na mchango unaotolewa na Kanisa mahalia.







All the contents on this site are copyrighted ©.