Ugonjwa wa Ebola ni tishio kwa usalama wa umma na unapaswa kushughulikiwa kimataifa!
Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Afya Duniani, WHO, DR. Margaret Chan, baada ya mkutano
wa siku mbili kuhusu dharura ya ugonjwa wa Ebola unaoendelea kuenea katika nchi kadhaa,
Afrika Magharibi, Ijumaa tarehe 8 Agosti 2014 ametangaza rasmi kwamba, ugonjwa wa
Ebola ni tishio kwa usalama wa umma na kwamba, ni janga linalopaswa kushughulikiwa
kimataifa!
Watalaam wa Shirika la Afya Duniani wametangaza kwamba, ugonjwa
huu unapaswa kushughulikiwa na kuratibiwa na Jumuiya ya Kimataifa, ili kuuzuia usienee
sehemu nyingine zaidi, kwani athari zake zinavuka mipaka ya nchi husika. Shirika la
Afya Duniani linatarajia kutoka maelekezo kwa nchi wanachama ili kuangalia namna ya
kuweza kuzuia ugonjwa wa Ebola usienee zaidi.
Takwimu zinaonesha kwamba, hadi
kufikia Ijumaa, tarehe 8 Agosti 2014, wagonjwa elfu moja wa Ebola wamekwishafariki
dunia. Hali ni mbaya nchini Liberia, Guinea na Sierra Leone. Watu kutokana na hofu
ya kuambukizwa na ugonjwa wa Ebola wanahofia hata kuwazika ndugu zao na kuwaacha barabarani,
hali ambayo ni hatari zaidi.
Liberia imetangaza hali ya hatari kutokana na
kuzuka kwa ugonjwa wa Ebola baada ya hatua za dharura zilizokuwa zimechukuliwa na
Serikali yake kwa kipindi cha majuma mawili, kushindwa kudhibiti kuenea kwa ugonjwa
wa Ebola. Watu katika huduma zisizo za lazima kwa muda wa siku thelathini watapaswa
kubaki majumbani mwao.