Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 19 ya Kipindi cha Mwaka A wa Kanisa
Mpendwa msikilizaji wa Neno la Mungu, leo tunatafakari pamoja masomo Dominika ya 19
ya mwaka A wa Kanisa. Tunaalikwa kugundua sura ya Mungu katika Kristo mfufuka ambaye
anatuonesha uwezo na nguvu ya Mungu Baba katika upole na unyenyekevu.
Tukiongozwa
na Nabii Eliya tunamwona Mungu aliye mnyenyekevu. Hata hivyo ili nabii afikie hapo
kwanza anaonekana kuwa mtu aliyekata tamaa baada ya kazi yake ya unabii kuonekana
kutozaa matunda mapema. Yuko katikati ya Waisraeli ambao wamemwacha Mungu na kuchukua
tamaduni za kipagani. Anatarajia Mungu awaadhibu hawa kwa nguvu lakini Mungu hatendi
hilo.
Mawazo haya yanajionesha katika nabii pale mlimani Horeb anapotarajia
Mungu ajioneshe katika alama ya upepo wa nguvu, ngurumo na moto mkali, lakini badala
yake Mungu anajionesha katika upepo mtulivu na mwanana! Anajifunua kwa nabii Eliya
ili atoke katika mtizamo wa kipagani na kuingia katika mapenzi ya Mungu.
Mpendwa
sisi tuna picha gani juu ya Mungu? Wakati fulani naona tunayo picha ya Mungu apatilizaye
wadhambi wote. Zaidi wakati fulani tuko kama Wana wa Israeli ambao walimkataa Masiya
kwa sababu hakuja kwa mabavu badala yake alikuja amepanda mwanapunda! Walitaraji awaondoe
katika utawala wa kirumi kwa nguvu za kivita lakini hakuwa hivyo na matokeo yake walimkataa
na kumwua! Kwa sababu hiyo Mtume Paulo anawasikitikia Waisraeli, anashangaa kwa nini
hawaoni zawadi hiyo kubwa ya kuja kwa mkombozi katikati yao! Mpendwa kuweni macho
ili mshangao wa Mtakatifu Paulo usikupate!
Mwinjili Matayo anatusaidia kuelewa
Mungu wetu ni yupi. Anasema ni yule ambaye anasali pale mlimani, anayewaponya wagonjwa,
anayewalisha wenye njaa. Zaidi Mungu ni nguvu dhidi ya mwovu shetani. Jambo hili linajionesha
pale Kristo anapotembea juu ya bahari. Kwa watu wa kale bahari ni kielelezo cha shetani
na hivi kutembea juu ya bahari ni kumkanyaga shetani na nguvu zake. Kumbe Kristu ni
ushindi dhidi ya vitisho vyote vya shetani.
Kristu aliye upendo haachi Kanisa
lake bila nguvu hiyo, kumbe anawakabidhi mitume nguvu hiyo ili wakanyage maovu wanaposimamia
taifa lake. Jambo hili liko wazi pale Kristo anapomwambia Mtakatifu Petro atembee
juu ya bahari. Hata hivyo haachi kuwaambia kuwa ikiwa imani itapungua mtazama kama
Mtakatifu Petro anavyozama, lakini mkiomba msaada wangu nitawaokoa na ndivyo mara
moja Mtakatifu Petro anaomba msaada wa Mungu na kuokolewa.
Mpendwa, katika
maisha yako umepewa nguvu ya kumkanyaga shetani kwa ubatizo, yafaa kuitumia daima
nguvu hiyo kubaki katika upendo wa Mungu na kuepuka kuzama katika ulimwengu kasi unaokuza
ubinafsi na utamaduni wa kujipenda zaidi, utamaduni uelekeao katika kifo.
Kwa
tafakari hii tunaalikwa kutambua kuwa Mapenzi ya Mungu ni tofauti na mapenzi yetu,
Mungu wetu ni mfufuka, ni mshindi dhidi ya dhambi, mwenye huruma kwa wote. Tumsifu
Yesu Kristo. Tafakari hii imeletwa kwenu na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.