2014-08-07 14:52:03

Mshikamano wa Papa Francisko kwa Wakristo huko Iraq!


Baba Mtakatifu Francisko anafuatilia kwa umakini na wasi wasi mkuu hali ya Wakristo huko Mashariki ya Kati, kutokana na habari za kutisha zinazoendelea kutolewa na watu mbali mbali hususan Kaskazini mwa Iraq. Waathirika wakuu ni Wakristo ambao wamelazimika kuyakimbia makazi yao kutokana na vita inayoendelea huko Iraq.

Wakristo wanateswa na kudhulumiwa, kiasi cha kulazimika kukimbia bila hata ya kuchukua mahitaji msingi. Baba Mtakatifu wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili tarehe 20 Julai 2014 alipenda kuonesha mshikamano wake wa dhati na Wakristo huko Iraq. Baba Mtakatifu anapenda kuwahikishia uwepo wake katika imani kwa Kristo aliyeshinda dhambi na mauti!

Baba Mtakatifu anaendelea kuungana na viongozi wa kidini na watu wote wenye mapenzi mema, ili kuendelea kumwomba Roho Mtakatifu ili awasaidie kupata zawadi ya amani. Baba Mtakatifu anaiomba Jumuiya ya Kimataifa, kusaidia mchakato wa kusitisha vita na madhulumu dhidi ya Wakristo; kwa kuwasaidia wakimbizi na wahamiaji wanaotafuta hifadhi katika maisha yao. Hili ni kundi la watu ambalo linahitaji mshikamano wa upendo.

Baba Mtakatifu anasema Padre Federico Lombardi anawaombea watu wote, ili Mwenyezi Mungu, kisima cha amani aweze kuamsha ndani ya watu kiu ya kutaka kuanzisha mchakato wa majadiliano na upatanisho. Baba Mtakatifu anasema, ubaya hauwezi kushindwa kwa njia ya ubaya. Vita inashindwa kwa njia ya amani.







All the contents on this site are copyrighted ©.