Rasimu ya Katiba ya Tanzania kujadilika kwa siku 60!
Bunge Maalum la Katiba limepitisha azimio la mapendekezo marekebisho ya baadhi ya
Kanuni za Bunge Maalum la Katiba ili kuwezesha kujadili Rasimu ya Katiba kwa muda
siku 60 za nyongeza na tatu zilizobakia. Marekebisho hayo yamepitishwa kufuatia Mwenyekiti
wa Kanuni na Haki za Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Pandu Ameir Kificho kuwasilisha
mapendekezo ya kanuni hizo mapema Jumanne katika Bunge hilo mjini Dodoma mara baada
ya kuanza kikao cha 30.
Azimio hilo, limepitishwa baada ya baadhi ya wajumbe
kuchangia hoja hiyo na kuungwa mkono, ambapo uamuzi huo ulitangaza na Mwenyekiti wa
Bunge hilo, Mhe. Samuel Sitta. Mhe. Sitta alisema Bunge hilo, litaanza kujadili rasimu
ya Katiba Mpya katika kamati 12 kuanzia tarehe 6 Agosti, mwaka huu kwa muda wa siku
15 yaani hadi Agosti 27, mwaka huu.
“ Hivi sasa watumishi wa Bunge na Sekretarieti
wanaweka nyezo zote za kupitia , ambapo pia Katibu wa Bunge Maalum la Katiba yupo
nao anashughulikia suala hili pamoja na kamati ndogo ili kuwezesha kazi hii kufanyika
bila bughuza,” alisema Mhe. Sitta. Aliongeza kwamba baada ya hapo kutakuwa na siku
tatu kwa kamati kukamilisha Rasimu zao za Katiba.
“ Kamati zinatakiwa kutumia
sekretarieti ndogo kuandika sura wasisubiri hadi Agosti 28, mwaka huu. Tumeongeza
Idadi ya wataalamu katika kila sekretarieti ndogo,”alisisitiza. Aidha Mhe. Sitta alisema
kutokana na marekebisho ya Kanuni ya 32 kifungu cha 2 kinachosema kamati kubadilisha
sura za rasimu na sura, hivyo zinatakiwa kutumia muda wa siku saba kupendekeza sura
mpya kuanzia Agosti 6, mwaka huu hadi Agosti 13, mwaka huu.
Akizungumzia kuhusu
maudhurio ya wajumbe wa Bunge hilo, alisema watakiwa kutia saini kwenye maudhurio
hayo na hakuna kusainiana kila mtu atatia saini mwenyewe. Mhe .Sitta akifafanua kuhusu
utaratibu wa kutoa taarifa za kamati kwa vyombo vya habari alisema utatolewa.
Alisema
Bunge hilo litarejea Septemba 2, mwaka huu baada ya kukamilisha kazi za kamati. Bunge
hilo limeanza vikao vyake kwa mara nyingine Jumanne tarehe 5 Agosti, baada ya kuairishwa
Aprili 25, mwaka huu.