Vijana wa kizazi kipya wanapata taabu sana kusikiliza sauti ya Mungu inayowaita kujitosa
kimasomaso kwa ajili ya kumtumikia Yeye na Jirani zao, kwa njia ya miito mitakatifu
ndani ya Kanisa. Ni vijana ambao wametekwa na makelele mengi kiasi kwamba inakuwa
vigumu kuweza kupambanua sauti ya Mungu na makelele yanayowazunguka, kwani wakati
mwingine wanakumbana na utupu katika maisha yao ya ujana.
Kumbe, jambo
la msingi ni kuwasaidia vijana hawa kuona ile njia ya imani, kwa kuwasikiliza kwa
makini na kuwaongoza pole pole katika hali ya ukimya, kwani Mungu daima anazungumza
na watu wake kwa njia ya ukimya, katika undani wa maisha ya mwanadamu.
Hii
ni changamoto ambayo imetolewa na wajumbe waliokuwa wanahudhuria mkutano wa kimataifa
ulioandaliwa na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya kuhusu miito.
Wajumbe wameshirikisha uzoefu na mang’amuzi yao katika kuwasindikiza vijana kusikiliza
na hatimaye, kuitambua sauti ya Mungu inayowaalika kujisadaka kwa ajili ya Mungu na
Kanisa lake.
Kongamano hili limefanyika hivi karibuni Jimboni Varsavia, Poland.
Kongamano la miito kwa mwaka 2015 litaanza kushika kasi hapo tarehe 6 hadi 9 Julai
2015 na litafanyika mjini Prague. Kauli mbiu ya kongamano la mwaka huu ilikuwa ni
“Elimu inayojikita kwa Yesu kwa ajili ya huduma kwa miito nyakati hizi”.
Ni
kongamano ambalo limewashirikisha wakurugenzi wa miito na wadau mbali mbali wanaojihusisha
katika kuwasaidia vijana kusikia sauti ya Mungu inayowaalika kujisadaka kwa ajili
ya Kristo na Kanisa lake. Wajumbe wameonesha wasi wasi wao kutokana na kuendelea kupungua
kwa miito ya maisha ya Kipadre na Kitawa Barani Ulaya. Ushiriki wa waamini katika
maisha na utume wa Kanisa unaendelea kufifia mwaka hadi mwaka.
Hapa wajumbe
wanasema, kuna haja ya kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Uinjilishaji mpya kwa
njia ya ushuhuda wa maisha unaodhihirisha imani tendaji katika uhalisia wa maisha.
Vijana wafundishwe kujenga na kudumisha utamaduni wa watu kukutana kama anavyokazia
Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wa Kanisa. Ushuhuda wa imani tendaji
ni kati ya mambo ambayo yanaweza kuleta mvuto na mashiko kwa vijana kuweza kusikia
na hatimaye, kujisadaka kwa ajili ya Mungu na jirani. Hapa Kristo anapaswa kupewa
kipaumbele cha kwanza katika maisha na utume wa Kanisa.
Uinjilishaji mpya
ndiyo dhana inayopaswa kufanyiwa kazi kwa sasa badala ya kuendekeza mtindo wa maisha
wa zamani, ili kuwapatia vijana fursa ya kutambua na kuonja upendo wa Mungu katika
maisha, ili hatimaye, kufanya maamuzi magumu na endelevu, kwa ajili ya kujisadaka,
ili kushiriki katika maisha na utume wa Kanisa.
Haya ni maisha yanayoonesha
shukrani kwa Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya Upadre na Utawa. Vijana waelimishwe na kuelekezwa
umuhimu wa kujikita katika hija ya utakatifu wa maisha, kwa kukutana daima na Yesu
Kristo kwa njia ya Sala, Tafakari, Sakramenti na Matendo ya huruma.
Imehaririwa
na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.