2014-08-04 08:48:23

Makanisa kujadili athari za mabadiliko ya tabianchi!


Baraza la Makanisa Ulimwenguni kuanzia tarehe 21 hadi tarehe 22 Septemba 2014, litafanya mkutano kuhusu mabadiliko ya tabianchi utakaowahusisha viongozi wa kidini wapatao 30, huko New York, Marekani. Mkutano huu wa viongozi wa kidini unapania kutoa msukumo na changamoto kwa viongozi wa kisiasa kulivalia njuga pasi na utani tatizo la mabadiliko ya tabianchi linaloendelea kusababisha majanga kwa maisha ya watu na mali zao. RealAudioMP3

Mkutano huu utafanyika siku chache kabla ya viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa kuanza kushiriki katika mkutano ulioitishwa na Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon, ili kupembua kwa kina na mapana mikakati inayopaswa kuchukuliwa na Jumuiya ya Kimataifa katika kupambana na athari zinazosababishwa na mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuweka sheri itakayowabana ifikapo mwaka 2015.

Ni matumaini ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwamba, mchango wao utawaza kusikiwa na kufanyiwa kazi na Jumuiya ya Kimataifa katika mkutano wa mabadiliko ya tabianchi uliopangwa kufanyika Mwezi Desemba, 2014 huko mjini Lima, nchini PerĂ¹ na baadaye mjini Paris, Ufaransa kunako mwa 2015. Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika mikutano hii linapenda kudai haki msingi za binadamu.

Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwa zaidi ya miongo miwili limeendelea kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, lakini wakati huu madhara ya mabadiliko ya tabianchi yamefikia kiwango cha hali ya juu kabisa. Umefika wakati kwa viongozi wa kisiasa kuweka uwiano wa kile wanachozungumza na utekelezaji wa maamuzi haya, jambo linalohitaji ujasiri na maamuzi ya busara. Viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa katika maadhimisho ya mkutano wa mabadiliko ya tabianchi huko New York, Marekani, wanapaswa kukumbushwa wajibu wao msingi wa kimaadili, unaopaswa kufanyiwa kazi.

Baraza la Makanisa Ulimwenguni, linayataka Makanisa wanachama kuhakikisha kwamba, yanajifunga kibwebwe kulinda na kutunza mazingira, kwa kuwa na mikakati ya pamoja, itakayoiwezesha dunia, kuwa ni mahali bora zaidi pa kuishi kwa kuwarithisha vijana wa kizazi kipya mazingira bora zaidi, kuliko mwelekeo wa sasa unaoendelea kukatisha watu tamaa ya maisha kutokana na madhara makubwa ya mabadiliko ya tabia nchi.








All the contents on this site are copyrighted ©.