2014-08-02 08:55:02

Familia ya Kikristo ni chemchemi ya maisha mapya!


Mtindo wa mawasiliano unaofanywa na Baba Mtakatifu Francisko na Maadhimisho ya Sinodi mnaalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia ni kati ya mada kuu zilizochambuliwa hivi karibuni na wadau na wasemaji wakuu wa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, katika mkutano wake uliofanyika mjini Lisbon, Ureno, kwa mwaliko wa Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ureno. RealAudioMP3

Padre Paul Wuthe, msemaji mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Austria, akiwasilisha mada yake kama sehemu ya utangulizi wa mkutano huu, amewawezesha wadau na wasemaji wakuu wa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, kufanya upembuzi yakinifu kuhusu mtindo wa mawasiliano unaotumiwa na Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wake kwa Kanisa la Kristo. Wajumbe wanakiri kwamba, Baba Mtakatifu amekuwa ni kati ya “vigogo” katika vyombo vya mawasiliano ya jamii sehemu mbali mbali za dunia. Ni kiongozi ambaye amekuwa na mvuto mkubwa kwenye mitandao ya kijamii.

Lakini ikumbukwe kwamba, mtindo wake wa mawasiliano ni sehemu ya maisha yake ya kawaida yanayojengeka katika maneno, lakini zaidi kwa njia ya ushuhuda wa maisha ambayo kwayo anajitahidi kuvunja kuta za utengano kati yake na Watu wa Mungu. Ni kiongozi anayetaka kuwakumbatia wote, ili kuwaonjesha huruma na upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Baba Mtakatifu anaonesha kwa njia ya matendo ukweli wa maisha yake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, fursa na changamoto kwa Mama Kanisa kujikita katika majadiliano ya kina na walimwengu.

Wajumbe wa mkutano huu wanakiri kwamba, Baba Mtakatifu Francisko kwa mtindo wa maisha yake anaendelea kuwagusa wengi kutoka katika undani wa mioyo yao, lakini pia ameleta mwamko mpya miongoni mwa waandishi na vyombo vya habari kitaifa na kimataifa kuanza kuona mchango wa Kanisa katika ustawi, maendeleo na mafao ya wengi, ikilinganishwa na miaka kadhaa iliyopita, ambako habari za Kanisa zilionekana kutokuwa na mashiko wala mvuto katika vyombo vya habari! Kwa hakika wanasema, Papa Francisko ni kiboko yao!

Wajumbe wanaonya kwamba, kuna haja ya kuwa waangalifu sana kutokana na mtindo wa mawasiliano yanayojikita katika maisha na utume wa Baba Mtakatifu Francisko. Ni kiongozi anayezungumza kidogo, kiasi kwamba, watu wasipokuwa makini na kile anachozungumza, wanaweza kujikuita kwamba, wanapotoshwa na vyombo vya habari ambavyo kwa sasa vinakimbilia na kufuatilia mambo katika ufupi wake na kwa haraka.

Huu ndio utamaduni unaofanyiwa kazi na vyombo vya mawasiliano ya kijamii! Kumbe, kwa vyombo vya mawasiliano vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa, havina budi kuhakikisha kwamba, vinaendelea kutangaza maisha na utume wa Kanisa zima, kwa kujikita katika kweli za Kiinjili na hata wakati mwingine, kwenda kinyume ni vyombo vikuu vya upashanaji habari, ili kuondokana na mwelekeo mfinyu unaoweza kuugeuza mfumo wa upashanaji habari wa Kanisa kujikita katika maisha ya mtu!

Mkutano wa wadau na wasemaji wakuu wa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, ulipata baraka ya uwepo wa Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican, gwiji katika masuala ya habari, mtu ambaye kwa hakika ana uzoefu na mang’amuzi makubwa katika tasnia ya habari ndani na nje ya Kanisa.

Kardinali Lorenzo Baldisseri, Katibu mkuu wa Sinodi ya Maaskofu ameshiriki pia katika mkutano huu, ili kuwafunda wasemaji wakuu wa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, kujiandaa kikamilifu katika maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu familia, inayoadhimishwa hatua kwa hatua, kwa kuwashirikisha Watu wa Mungu. Maadhimisho haya yalizinduliwa kwa kuwashirikisha waamini na watu wenye mapenzi mema katika kujibu maswali dodoso kuhusu tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.

Hapa Kardinali Baldisseri anasema, si lengo la Kanisa kufanya utafiti kuhusu maisha ya ndoa na familia kwa njia ya maswali dodoso, bali hii ni sehemu ya mchakato wa utamaduni wa Kanisa kusikiliza kwa makini mchango unaotolewa na watoto wake, ili hatimaye, kuibuka na mbinu mkakati wa shughuli za kichungaji zinazotekelezwa na Mama Kanisa, kwa kukabiliana na changamoto hizi kwa imani na matumaini, ili kuendelea kutangaza Injili ya Familia kwa watu wa mataifa, bila woga wala makunyanzi!

Sehemu ya pili ya Maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu familia ni hati ya kutendea kazi itakayotumiwa na Mababa wa Sinodi, hati ambayo inajulikana kama “Instrumentum Laboris” ambayo imezinduliwa mjini Vatican hapo tarehe 26 Juni 2014. Hati hii itatumiwa na Mababa wa Sinodi itakayoadhimishwa mjini Vatican kuanzia tarehe 5 hadi 19 Oktoba 2014. Awamu ya Pili ya Maadhimisho ya Sinodi hii yanatarajiwa kufanyika kunako mwaka 2015, Sinodi itakayoibua mbinu mkakati wa shughuli za kichungaji kwa familia ya binadamu.

Hapa Kanisa linapenda kukazia ukweli na uwazi, utume na uadilifu katika kusimamia kweli za Kiinjili, kwa kusikiliza na kuamua kwa ujasiri, ili kuwatangazia watu wa mataifa Injili ya Familia, chemchemi ya matumaini na maisha mapya. Mababa wa Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu Familia watato mwelekeo wa Kanisa kuhusu maisha ya ndoa na familia, changamoto ambayo imevaliwa njuga na Baba Mtakatifu Francisko tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki.

Wasemaji wakuu wa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya wamekumbushwa kwamba, hii si Sinodi ya Maaskofu wa Bara la Ulaya, bali ni Sinodi inayolishirikisha Kanisa zima, kumbe ni kipindi cha kusali, kutafakari na kushirikishana tunu mbali mbali za maisha ya ndoa na familia.

Kuna haja anasema Kardinali Baldisseri kuwa na mwelekeo mpana zaidi badala ya kujikita katika masuala magumu na nyeti katika maisha ya ndoa na familia na hatimaye kupuuzia ushuhuda unaotolewa na Familia ya Mungu katika maisha ya ndoa na familia, kwani licha ya matatizo, changamoto na fursa mbali mbali zilizopo, kuna familia ambazo kweli zimekuwa ni kielelezo cha Injili ya Familia katika uhalisia wa maisha yao ya kila siku, hawa ni watu wakupongezwa na kutiwa shime, ili waweze kusonga mbele kwa imani na matumaini.

Mkutano wa wasemaji wakuu kutoka Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, ulihudhuriwa pia na Bwana Benedict Assorow, msemaji mkuu wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM.








All the contents on this site are copyrighted ©.