2014-08-01 09:17:28

Vunjilieni mbali kuta za utengano, ili kujenga na kuimarisha upendo na msamaha!


Kardinali Rodriguez Maradiaga, Rais wa Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis katika tafakari yake ya kina kuhusu vita na machafuko yanayoendelea huko Mashariki ya Kati, anamwomba Yesu asaidie watu kuvunja kuta za kinzani, ili kujenga na kuimarisha mshikamano wa upendo, kwa kujifunza kutoka kwa jirani zao, huku wakipania kuwasamehe wale waliowakosea.

Ni maneno ya Mtakatifu Yohane wa XXIII katika Waraka wake wa kichungaji Amani Duniani, Pacem in Terris aliyoyatoa zaidi ya miaka hamsini iliyopita, lakini bado yana umuhimu wa pekee wakati huu ambapo kuna vita na kinzani zinazoendelea sehemu mbali mbali za dunia. Kuna zaidi ya watu millioni mbili ambao wamekumbwa na madhara ya vita huko Mashariki ya Kati. Ni watu ambao hawana uhakika wa usalama wa maisha yao, watu wasiokuwa na hatia wanaendelea kupoteza maisha yao huko Ukanda wa Gaza, kiasi kwamba, matumaini ya kupata amani yanaendelea kufifia kila kuchwapo!

Jambo la kustikisha ni kuona kwamba, uwanja wa vita ni sehemu ambayo imesheheni watu na hospitali zimefurika kwa watu waliojeruhiwa na maiti za watu wasiokuwa na hatia. Watu wanalipuliwa wakiwa shuleni, mahali ambapo wamekimbilia kutafuta usalama wa maisha yao.

Caritas Internationalis imeziomba pande zinazohusika kusitisha vita, kama sehemu ya kwanza ya mchakato unaopania ujenzi wa amani inayojikita katika majadiliano ya kina huko Mashariki ya Kati. Ni mwanzo wa hija ngumu ya upatanisho inayokijita katika maisha ya mtu binafsi, changamoto kwa Israel na Hamas kuweka silaha chini na kuanza mchakato wa majadiliano. Hii ni vita ya tatu katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.

Wapalestina wanaishi katika mazingira magumu kwani kwa sehemu kubwa maisha yao yanategemea misaada kutoka katika Jumuiya ya Kimataifa na kwamba, hakuna fursa za ajira. Kuna haja ya kuwapatia wananchi wa Palestina fursa ya kuokoa maisha yao kwa kujikita katika mchakato wa ujenzi wa amani inayokumbatiwa kwa ujasiri, majadiliano na kuheshimiana. Caritas inaombea amani na utulivu huko Mashariki ya Kati na inaendelea kutoa msaada wa hali na mali hata kwa kuhatarisha maisha ya wafanyakazi wake.

Jumuiya ya Kimataifa inafanya kumbu kumbu ya miaka mia moja tangu ilipoanza vita kuu ya kwanza ya dunia, hata katika shida na mahangaiko ya wananchi wa Palestina na Israeli, Kardinali Oscar Rodriguez Maradiaga anasema, mioyo ya wananchi hawa inapaswa kuwa huru, ili kukumbatia misingi ya haki na amani.







All the contents on this site are copyrighted ©.