Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili iliyopita tarehe 27 Julai 2014 akiwa kwenye Uwanja
wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, alizungumzia mifano iliyotolewa na
Yesu kuhusu Ufalme wa Mungu, unaoweza kumfikia mwamini pasi na kutarajia au baada
ya kufanya hija ya kipindi kirefu katika maisha, anapogundua hazina hii, anauza kila
kitu ili kuweza kuipata.
Hivi ndivyo mambo yalivyo hata katika Ufalme wa Mungu.
Kwa mtu anayemfahamu, aliyebahatika kukutana na Yesu, anabaki akiwa amepigwa na bumbuwazi
kutokana na unyenyekevu wake, ukweli na uzuri. Hii ni changamoto kwa waamini kumtafuta
Yesu kwani Yesu ndiye hazina ile kubwa ambayo imefichika machoni pa wengi. Watakatifu
na watu wengi waliobahatika kusoma na kutafakari Injili wamebahatika kumgundua na
kukutana na Yesu katika maisha yao, kiasi kwamba, wametubu na kumwongokea Mungu.
Hawa
ni kama vile akina Mtakatifu Francisko wa Assis aliyeachana na malimwengu baada ya
kukutana na Yesu akagundua Ufalme wa Mungu akaamua kuukumbatia. Yesu anazungumza na
mtu kutoka katika undani wake na kumwezesha mwamini kubadili mwelekeo wa maisha yake
na kuwa ni mtu mpya zaidi. Kwa mwelekeo huu, mwamini anapata mambo msingi, mwanga
na faraja hata katika shida, masumbuko na kifo, changamoto kwa waamini kujenga utamaduni
wa kujisomea Neno la Mungu, ili kuweza kukutana na Yesu ambaye ndiye hazina kubwa
iliyofichika, ili kumpatia nafasi Mwenyezi Mungu kuweza kutawala katika maisha yao.
Baba
Mtakatifu Francisko anawakumbusha waamini kwamba, Mungu ni upendo, ni chemchemi ya
amani na furaha kwa wote na huu ndio utashi wa Mungu kwa kila mwanadamu ndiyo maana
amemtoa Mwanaye wa pekee Yesu Kristo ili azaliwe, ateswe na kufa Msalabani kwa ajili
ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti na hivyo kimkirimia
maisha ya uzima wa milele. Kumpata na hatimaye kumkumbatia Yesu ni chemchemi ya furaha
ya maisha ya Kikristo.
Waamini wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuhakikisha
kwamba, wanatolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake katika uhalisia
wa maisha ya kila siku. Baba Mtakatifu anamwomba Bikira Maria awaombee waamini ili
Ufalme wa Mungu uweze kufika hapa duniani, Ufalme unaojikita katika upendo, haki na
amani.