2014-07-28 12:01:14

Marehemu Kardinali Francesco Marchisano alijisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake!


Baba Mtakatifu Francisko amemtumia salam za rambi rambi Askofu mkuu Cesare Nosiglia wa Jimbo kuu la Torino kutokana na kifo cha Kardinali Francesco Marchisano, aliyefariki dunia, Jumapili tarehe 27 Julai 2014. Baba Mtakatifu anapenda kuwahakikishia wote walioguswa na msiba huu uwepo wake wa karibu, katika kipindi hiki cha maombolezo.

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu anamkumbuka Marehemu Kardinali Marchisano aliyejisadaka kwa ajili ya shughuli mbali mbali za kitume mjini Vatican, hasa zaidi katika Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki na baadaye akateuliwa kuwa Mhudumu mkuu wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican na mwishoni kabisa, alikuwa ni Rais Idara ya Kazi ya Vatican.

Marehemu Kardinali Marchisano anaacha ushuhuda mkubwa wa maisha ya kiongozi aliyejitosa kimasomaso kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, kama Padre na Askofu, daima akiwa makini kutekeleza mahitaji ya waamini wake, makini katika utunzaji wa sanaa na utamaduni. Baba Mtakatifu anamwombea Marehemu ili Mwenyezi Mungu aweze kuipokea roho ya Marehemu katika raha na amani ya milele. Baba Mtakatifu anapenda kuchukua fursa hii kutoa baraka zake za kitume kwa wote wanaoomboleza kifo cha Kardinali Marchisano.

Wakati huo huo, Mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa, Monsinyo Guido Marini anasema kwamba, Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumwombea Marehemu Kardinali Francesco Marchisano, itaadhimishwa Jumatano tarehe 30 Julai 2014, majira ya saa 2:00 za asubuhi kwa saa za Ulaya na kuongozwa na Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali. Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuongoza Ibada ya Mazishi.







All the contents on this site are copyrighted ©.