Askofu Amon Mwenda wa Dayosisi ya Ruvuma, Kanisa la Kiinjili la Kiluteri Tanzania
asimikwa rasmi!
Waziri mkuu Mizengo Pinda amewaonya Watanzania kuwa makini na watu wanaotumia rushwa
ili kupata nafasi za uongozi na hasa kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba,
2015. Ametoa onyo hilo Jumapili, Julai 27, 2014 wakati akizungumza na mamia ya waamini
na viongozi mbalimbali waliohudhuria ibada ya uzinduzi wa Dayosisi mpya ya Ruvuma
ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) na kuwekwa wakfu Askofu Amon Mwenda
aliyeteuliwa kuongoza dayosisi hiyo.
“Ninawasihi wananchi wawe makini na viongozi
wanaopenda kutoa rushwa hasa katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye uchaguzi mkuu.
Kama mtu ana nia ya kweli ya kuongoza ni kwa nini atumie fedha ili kupata nafasi ya
uongozi?,” alihoji. “Tatizo ni kwamba hata wananchi hivi sasa wanakubali kupokea kile
kinachotolewa na wagombea. Atakuja huyu atakupa hiki na mwingine naye atakupa kile,
lakini ujue akiingia madarakani anaanza kurudisha haraka vile alivyowagawia,” alisema.
Aliwaonya
wananchi kuwa makini ili wasije wakageuzwa mtaji wa kuwanufaisha watu binafsi. “Tukikubali
kutumika ni sawa tutapata viongozi wakati wa uchaguzi, lakini watakuwa ni wale wasio
na hofu ya Mungu, wenye kujali maslahi yao kuliko ya wananchi waliowachagua,” aliongeza.
Aliwaomba viongozi wote wa dini waliohudhuria sherehe hizo pamoja na waumini wote
waendelee kuliombea Taifa ili Mungu aliepushe na janga hilo la watu kupenda rushwa.
Alitumia fursa hiyo pia kuwaomba wazidi kuuombea mchakato wa kupata Katiba mpya ili
wabunge wote warejee ndani ya Bunge na kuikamilisha kazi waliyoianza.
Alimwomba
Askofu huyo mpya apokee jukumu hilo kwa mikono miwili na kumuahidi kuwa kama Serikali
watakuwa naye bega kwa bega kuwaongoza Watanzania walioko kwenye dayosisi yake. Dayosisi
hiyo mpya inahusisha mkoa wote wa Ruvuma na wilaya ya Ludewa eneo ambalo lina ukubwa
wa kilometa za mraba 72,630. Kati ya hizo km. za mraba 64,233 ni za mkoa wa Ruvuma
na km. za mraba 8,397 ni za wilaya ya Ludewa.
Mapema, akitoa hotuba yake ya
kwanza mara baada ya kusimikwa rasmi, Askofu Mwenda alisema dayosisi mpya ya Ruvuma
imezaliwa katika kipindi chenye changamoto nyingi za kidunia na utandawazi ukiwemo
mmong’onyoko mkubwa wa maadili. Hata hivyo, akiainisha malengo ya dayosisi hiyo ambayo
anakuwa Askofu wake wa kwanza, Askofu Mwenda alisema mbali ya kufundisha Neno la Mungu,
dayosisi hiyo itahimiza ufanyaji kazi ili wakazi wake wawe na akiba ya chakula cha
kutosha.
Alisema watashirikiana na Serikali na wadau wa ndani najje katika
kutoa huduma za kijamii hasa elimu na afya. Aidha alisema atakabiliana na changamoto
za sasa ambazo alizitaja kuwa ni mmomonyoko wa maadili, rushwa, mauaji ya albino,
unajisi wa watoto na ubakaji wa wanawake.
Akitoa shukrani kwa niaba ya waumini
wa kanisa hilo, Askofu Mkuu wa KKKT, Dk. Alex Malasusa alisema Kanisa lingependa kupata
viongozi ambao ni wacha Mungu. Akirejea mahubiri yake, Askofu Malasusa alisema inashangaza
kuona kuna baadhi ya watu wanagombea nafasi za uongozi lakini hawana mapenzi na Mungu
aliyewaumba watu anaotaka kuwaongoza.
“Bila kujali imani ya mtu, tunatamani
tungepata kiongozi ambaye anamcha Mungu. Awe anapenda kuhudhuria ibada. Awe anampenda
Mungu ndipo atawapenda watu anaowaongoza,”alisisitiza.