Baada ya kutafakari Injili juu ya ngano na magugu Dominika iliyopita, Injili ya leo
– inatualika tutafute ilipo hazina na lulu ya kweli. Hapa Yesu Kristo anatamka mwenyewe
juu yake na ujio wake ulimwenguni. Hivi tunaalikwa tutumie nafasi hii njema ya wokovu.
Ni muda wa kuamua. Hazina, yaani Kristo, yupo. Tusipoteze nafasi hiyo. Hii
mifano miwili hazina na lulu ni mwaliko wa kuutafuta huo ufalme. Tungeweza kujiuliza
mara moja – Je, sisi tunatafuta nini au tumewekeza wapi? Katika maisha ya kawaida
twaona kuwa tumewekeza sana kaitka mambo mengi kwa mfano kwenye bima ya maisha, ya
afya nk. Ni sawa na sahihi kabisa. Na bima hizi huwa ni kwa ajili ya kulinda maisha
ya kawaida ya mtu awapo duniani na pengine baada ya kifo wale wanaobaki waweze kupata
sehemu ya mali ya marehemu.
Bibi mmoja aliyekuwa tajiri – alipofariki bahati
nzuri alifika mbinguni. Ila alipata sehemu ndogo ya kukaa na pembezoni. Akamlalamikia
malaika aliyemwongoza kwenda sehemu hiyo. Unanileta mahali hapa? Mbona mimi huko duniani
nilikuwa na kila kitu na nilikapaa mahali pa fahari? Malaika kwa unyenyekevu akamjibu
– tafadhali ridhika na ulichopata. Vile vifaa vya ujenzi ulivyotuma huku mbinguni
vilitosha kutengeneza tu kiti hiki kidogo ambapo ndiyo mahali pako pa kujisetiri milele.
Ridhika na ulichotoa. Malaika akaenda zake.
Leo hii tunaalikwa tuwekeze kwenye
bima ya ufalme wa mbinguni. Tukumbuke kuwa ufalme wa mbinguni ni bima dhidi ya kifo.
Yesu atuambia waziwazi, aniaminiye hata kama akifa, ataishi milele. Hivyo twaelewa
vizuri mwaliko wake – uza vyote na kuutafuta kwanza ufalme. Kuwa tayari kutoa sadaka
yo yote kwa ajili ya huo ufalme wake.
Leo tunaulizwa – katika yote ninayotamani
katika maisha – ni kipi nathamini zaidi au nahitaji zaidi? Injili inaweka wazi– kwanza
ufalme wa mbinguni – Mt. 6:33 –basi, kwanza utafuteni ufalme wa Mungu na uadilifu
wake, na hayo yote mtaongezewa. Ufalme wa Mungu ni utawala wa Mungu mioyoni mwetu,
katika maisha yetu, nyumbani kwetu, katika jamii na katika ulimwengu wetu. Anayepata
ufalme wa Mungu amepata yote. Ndiyo maana inalinganishwa na hazina bora iliyopatikana
shambani au lulu ya thamani kubwa. Msisitizo uko siyo kutafuta kwanza ufalme wa Mungu
pamoja na mengine yanayoambatana nayo lakini msisitizo uko katika kutafuta tu ufalme
huo.
Pengine somo la kwanza litupe changamoto tena leo – Sulemani akiwa mfalme
kijana alikuwa na mahitaji mengi sana. Alihitaji utajiri, jeshi kubwa na imara, umaarufu,
usalama, ustawi, maisha marefu, furaha n.k. Lakini katika nafasi aliyopewa na Mungu
ya kuomba – aliomba hekima. Alifahamu fika akiwa na hekima ya Mungu mengine yote yatawezekana.
Na Mungu anamhakikishia hilo 1 Waf. 3: 11-13 –Mungu akamwambia, kwa kuwa umeomba jambo
hili – wala hukujitakia maisha marefu, wala hukujitakia utajiri, wala hukuomba roho
za adui zako, bali umeomba hekima ya kujua kuhukumu, basi, tazama ninatenda kama ulivyosema.
Ninakupa moyo wa hekima na akili, hata kabla yako hakupatikana mtu kama wewe, na wala
baada yako hatainuka mtu kama wewe,. Hata mambo yale usiyoyaomba nimekupatia: utajiri,
heshima na utukufu kushinda wafalme wengine wote.
Sijui leo tungepata nafasi
kama ya Mfalme Sulemani tungeomba nini. Utajiri, mafanikio katika biashara? Maisha
mema na ya upendo thabiti? Je tungekuwa na hekima ya Sulemani kuomba hekima katika
maisha yetu ya kila siku? Ni ipi nafasi ya ufalme wa Mungu katika maisha yako? Tusisahau
kuwa ufalme wa Mungu si moja kati ya mambo tuyatamaniyo ila ndicho pekee tunachohitaji.
Mengine ni ziada.