2014-07-24 15:26:45

Sheria kudhibiti madhehebu ya kidini Burundi


Nchini Burundi katika kipindi cha miaka ishirini, idadi ya madhehebu ya kidini nchini humo imeongezeka maradufu kutoka madhehebu arobaini na tano hadi kufikia madhehebu mia sita, kiasi cha kuihamasisha Serikali ya Burundi kutafuta njia ya kudhibiti wimbi hili kubwa kwa kutunga sheria ambayo tayari imepitishwa na Bunge la Burundi. RealAudioMP3

Ili dhehebu la kidini liweze kutambulika rasmi kisheria nchini Burundi, halina budi kuwa na wafuasi walau mia tano na kama dhehebu hili linatoka nje ya nchi basi linapaswa kuwa na wafuasi walau elfu moja. Madhehebu ya dini nchini Burundi yamepewa kipindi cha miaka miwili, ili kuweza kurekebisha kasoro zilizopo na hatimaye, sheria iweze kuanza kushika mkondo wake, ili kudhibiti ongezeko la madhehebu ya kidini ambayo mengi yameonesha kuwa na msukumo wa kiuchumi zaidi, kuliko hata maisha ya kiroho.

Wachunguzi wa masuala ya kidini wanasema, kufumuka kwa amdhehebu haya kunawawezesha viongozi wake kuendelea kupata msaada wa raslimali fedha na hivyo kugeuza madhehebu haya kuwa kweli ni vitega uchumi na hivyo hata kushindwa kudhitiwa na Serikali. Takwimu zinaonesha kwamba, aslimia 75% ya wananchi wa Burundi ni waamini wa Kanisa Katoliki na kwamba, asilimia kati ya 3-4% ni waamini wa dini ya Kiislam na wengine waliobakia ni waamini wa Madhehebu mbali mbali ya Kikristo.

Wachunguzi wa mambo wanasema, sheria hii imekuja wakati ambapo Burundi inajiandaa kwa ajili ya kuanza mchakato wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika nchini humo kunako mwaka 2015. Madhehebu ya kidini yanaweza kuwa ni mwiba mkubwa katika mchakato wa uchaguzi huu ukitazamwa kwa jicho la kisiasa. Bado watu wanakumbuka mauaji ya waamini wa madhehebu ya Kikristo yaliyofanyika kunako mwaka 2013, mjini Businde, Mkoani Kayanza.

Wizara ya mambo ya ndani ya Burundi inasema kwamba, lengo la sheria hii ambayo imepitishwa hivi karibuni nchini Burundi ni kudhibiti wimbi la madhehebu ya kidini pamoja na kuimarisha ulinzi na usalama kwa wananchi wa Burundi. Ibada za madhehebu haya zinapaswa pia kufanyika katika maeneo yenye hadhi ya Ibada kwa ajili ya kumtukuza Mwenyezi Mungu na mwanadamu kutakatifuzwa. Imani ni chaguo la mtu binafsi na kwamba, uhuru wa kidini hauna budi kuheshimu pia haki msingi za wananchi wengine ndani ya Jamii.








All the contents on this site are copyrighted ©.