Wakristo Mashariki ya Kati, kamwe si watu wa kuja!
Kardinali Leonardi Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya
Mashariki anasema amani inapaswa kutawala na hivyo kushinda kishawishi cha matumizi
ya mtutu wa bunduki, jambo ambalo linaendelea kusababisha mateso makubwa kwa watu
wasiokuwa na hatia. Wakristo nchini Iraq wanadhulumiwa na kuteswa kumbe, kuna haja
kwa Jumuiya ya Kimataifa kusaidia juhudi za kusitisha mapigano huko Mashariki ya Kati,
ili amani ya kweli iweze kutawala kati ya watu.
Kardinali Sandri anaonesha
masikitiko yake makubwa kutokana na mateso ya watu wanaolazimika kuyakimbia makazi
yao kwa kuhofia usalama wa maisha na mali zao. Wakristo huko Mosul na Aleppo wanakabiliana
na madhulumu ya kidini, kwani nyumba na Makanisa yao yameharibiwa vibaya sana kutokana
na chuki za kidini. Hali hii inaonesha kwamba, huko Mashariki ya Kati usalama kwa
Wakristo ni kidogo sana, lakini kwa bahati mbaya, Jumuiya ya Kimataifa inaonekana
kutoguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya Wakristo huko Iraq na Mashariki ya Kati
katika ujumla wake.
Utu, maisha na heshima ya kila mtu vinapaswa kupewa kipaumbele
cha kwanza na kamwe vita si suluhu ya amani ya kudumu, bali ni chanzo na mwendelezo
wa watu kulipizana kisasi. Kardinali Sandri anapenda kuonesha mshikamano wake wa dhati
na viongozi wa Makanisa ya Mashariki ambao wameendelea kuwa bega kwa bega na waamini
wao katika kipindi hiki kigumu cha historia na maisha yao. Jambo la msingi ni watu
kupania kudumisha uhuru wa kuabudu sanjari na kuendeleza haki msingi za binadamu.
Wakristo
wanaoishi huko Mashariki ya Kati si watu wa kuja wala wageni, ni raia wenye haki na
dhamana katika nchi yao wenyewe, kumbe vitendo vya kuwanyanyasa na kuwabagua ni kinyume
cha sheria za nchi na haki msingi za binadamu. Wakristo wanapaswa kuendelea kuishi
katika maeneo yao, ili kuchangia katika ustawi na maendeleo yao: kiroho na kimwili.
Kwa
namna ya pekee kabisa, Kardinali Sandri anawakumbuka na kuwaombea Wakristo wanaoishi
Nchi Takatifu, Lebanon, Syria, Iraq na Misri, bila kuwasahau wahanga wote wa mashambulizi
ya kivita. Ni matumaini yake kwamba, Jumuiya ya Kimataifa itasaidia juhudi za kujenga
na kudumisha: uhuru, haki msingi za binadamu, upatanisho na amani ya kweli kati ya
wananchi wanaoishi huko Mashariki ya Kati. Watu wajenge utamaduni wa kuheshimiana,
kuthaminiana na kusaidiana kama ndugu na kwamba, chuki na uhasama wa kidini ni mambo
yaliyopitwa na wakati na wala hayana tija wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya
watu.
Wakristo wanayo haki kabisa ya kuishi huko Mashariki ya Kati ambako
ni chimbuko la Ukristo, yapata miaka elfu mbili iliyopita. Kardinali Leonardo Sandri
anawaomba waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuendelea kusali bila kuchoka kwa
ajili ya kuombea amani, utulivu na upatanisho huko Mashariki ya Kati. Wanamwomba Yesu
Kristo, Bwana wa amani, awasaidie kuendeleza moto wa matumaini hata katika mazingira
haya magumu na yenye kukatisha tamaa.