Familia, kiini cha Siku kuu ya Mtakatifu Anna kwa Mwaka huu
Tunu msingi za maisha ya ndoa na familia ni kiini cha tafakari kama sehemu ya maandalizi
ya Siku kuu ya Mtakatifu Anna, Mama yake Bikira Maria, ambayo kwa mwaka huu inaadhimishwa
kwa namna ya pekee kabisa, wakati huu Mama Kanisa anapoendelea kujiandaa kwa ajili
ya maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, yatakayofanyika
mjini Vatican kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba 2014.
Katika Parokia ya
Mtakatifu Anna iliyoko mjini Vatican, waamini wameanza Sala kwa ajili ya maandalizi
ya Siku kuu ya Mtakatifu Anna, kwa kusali na kuwaombea watoto, wanawake na wazee.
Padre Bruno Silvestrini, Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Anna mjini Vatican anasema
kwamba, kipindi hiki cha siku tatu hadi kilele cha maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu
Anna, waamini Parokiani hapo wanasali na kutafakari kuhusu tunu msingi za maisha ya
ndoa na familia. Ni kipindi cha kushuhudia Injili ya Familia, ili kurithisha tunu
hizi kwa vijana wa kizazi kipya.
Anasema, wanawake wajawazito wanaendelea
kusali kwa ajili ya kumwomba Mtakatifu Anna ili awasaidie kupata utulivu katika shida
na mahangaiko yao ya ndani, ili hatimaye waweze kujifungua salama kadiri ya mapenzi
ya Mungu na kuwalea watoto wao katika misingi ya Kikristo na utu wema.
Kilele
cha maadhimisho haya ni hapo tarehe 26 Julai 2014 kwa Sala na Ibada ya Misa takatifu
itakayoongozwa na Kardinali Angelo Comastri, Makamu Askofu, Mji wa Vatican. Ibada
hii itafanyika wakati wa mchana. Jioni majira ya saa 12:00, Kardinali Pietro Parolin,
Katibu mkuu wa Vatican ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Parokia ya Mtakatifu
Anna, ili kwa maombezi ya Mtakatifu Anna, wanawake wajawazito waweze kujifungua salama
na asaidie pia kulinda familia ambazo kwa nyakati hizi zinakabiliwa na misuko suko
ya maisha.