2014-07-22 09:33:41

Waonjesheni wagonjwa upendo na mshikamano!


Vingozi wa kidini nchini Uingereza wametoa tamko la pamoja kupinga muswada wa sheria unaotaka kuhalalisha mchakato wa kifo laini kwa kuwapatia msaada wa kitabibu wale wanaotaka kujinyonga, muswada ambao umeanza kujadiliwa nchini Uingereza. RealAudioMP3

Muswada huu unampatia uwezo wa kisheria daktari kutoa dawa itakayochochea kifo pole pole kwa wagonjwa wa muda mrefu au wale ambao wana magonjwa yasiyokuwa na tiba. Moja ya masharti ni kwamba, mgonjwa anapaswa kufanya maamuzi haya magumu kwa utashi kamili pasi na shuruti.

Viongozi wa kidini wanasema, maisha ya mwanadamu ni zawadi na tunu kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kumbe inapaswa: kupendwa, kulindwa na kuendelezwa. Huu ndio msingi thabiti wa sheria unaoweza kudumisha mahusiano mema katika jamii. Muswada wa sheria unaonesha mwelekeo tenge wa Jamii inayotakiwa nchini Uingereza, kwa kutozingatia uhai wa mwanadamu na kwamba, utu na heshima ya mtu inapimwa kutokana na mchango wake katika Jamii. Lakini kila mtu anapaswa kupendwa, kusaidiwa na kulindwa hata kama wakati mwingine mtu kama huyu anashindwa kujipenda na kujilinda mwenyewe.

Viongozi wa kidini nchini Uingereza wanasema kwa dhati kwamba muswada wa sheria unaojadiliwa nchini Uingereza kwa sasa una lengo la kumong’onyoa tunu msingi za maisha kwa siku za usoni, kiasi cha kushindwa kuheshimu na kuwalinda watu wake. Shauku ya mtu kutaka kukatisha maisha yake binafsi inaweza kuchangiwa na mambo mengi kutoka ndani na nje ya mtu husika. Muswada wa sheria utawatendea wanyonge na wagonjwa wa mgonjwa yasiokuwa na tiba, watu ambao wanapaswa kupendwa na kusaidiwa, lakini Jamii inawageuzia kisogo.

Viongozi wa kidini nchini Uingereza wanasema, kinachotakiwa hapa ni tiba makini kwa ajili ya wagonjwa walioko kufani pamoja na kuendelea kutoa msaada wa hali na mali kwa ndugu na jamaa wanaowauguza wagonjwa hawa, jambo ambalo linaonesha Jamii inayowajali watu wake na huko ndiko ambako Jamii inapaswa kuelekeza nguvu zake. Wagonjwa wanapaswa kuhudumiwa na wala si kusukumizwa kwenye tanuru la kifo. Dhamana ya maisha ya mtu iko mikononi mwa Mwenyezi Mungu peke yake.








All the contents on this site are copyrighted ©.