2014-07-21 11:08:33

CRS kuendelea kushikamana na Nchi za AMECEA katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo


Dr. Carolyn Woo, Mkurugenzi mtendaji na Rais wa Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki Marekani, CRS, katika mkutano wa kumi na nane wa AMECEA anasema kwamba, ushuhuda wa imani tendaji ni kati ya changamoto zinazopewa kipaumbele cha kwanza na Shirika hili katika mipango na mikakati yake na kwamba, wanapania kuendeleza na kudumisha mshikamano wa kidugu na AMECEA katika utekelezaji wa mikakati yake kama inavyofafanuliwa kwa kina na mapana katika Waraka wa kichungaji, Dhamana ya Afrika, Africae Munus.

CRS inatambua changamoto zinazoikabili nchi za AMECEA, ikiwa ni pamoja na kinzani za kidini, kisiasa, kijamii na kiuchumi; kuibuka kwa misimamo mikali ya kidini, majanga asilia, baa la njaa, ukosefu wa ajira sanjari na biashara haramu ya binadamu mambo yanayodhalilisha utu na heshima ya binadamu. Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki kwa kushirikiana na AMECEA linapenda kujielekeza zaidi katika kuwasaidia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kama kielelezo cha imani tendaji.

CRS linasubiri kusikia mikakati ya maendeleo ya AMECEA kwa kipindi cha miaka kumi ijayo, ili liweze kuchangia kwa hali na mali katika utekelezaji wake, katika masuala ya kiufundi na kifedha kama lilivyofanya kwa miaka mingine iliyopita. Ikiwa kama changamoto hizi hazitashughulikiwa kikanilifu, kuna hatari kwamba, kiwango cha maendeleo kilichofikiwa na Nchi za AMECEA kinaweza kuporomoka. CRS inapania kuendelea kuchangia utekeleza wa miradi mbali mbali ya maendeleo inayoibiliwa na Majimbo Katoliki kutoka AMECEA.

Ushirikiano huu unajikita kwa namna ya pekee katika changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kuhusu mshikamano wa upendo, na kuridhiwa na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM kunako mwaka 2012, mjini Kinshasa, DRC.







All the contents on this site are copyrighted ©.