2014-07-19 11:08:06

Vitendo vya kigaidi, misimamo mikali ya kidini na ukabila ni mambo yanayokwamisha maendeleo ya wengi Barani Afrika!


Askofu Eduardo Hiiboro wa Jimbo Katoliki Tombura-Yambio, lililoko Sudan ya Kusini, kwa niaba ya Baraza la Maaskofu Katoliki Sudan lililopewa dhamana ya kupembua mada inayohusu mazingira ya kitamaduni, kisiasa na kijaamii ambamo Kanisa linatekeleza dhamana na utume wake, amewakumbusha wajumbe wa mkutano mkuu wa AMECEA unaoendelea Jimboni Lilongwe, Malawi kwamba, kuna nchi kumi na saba Barani Afrika ambazo zinakabiliwa na migogoro, kinzani na vita.

Kutokana na hali kama hii, Kanisa halina budi kuwa ni sehemu ya mchakato wa majadiliano yanayolenga kutafuta suluhu ya amani ya kudumu Barani Afrika. Kanisa lisaidie kuhakikisha kwamba, sera za kijamii, kisiasa na kiuchumi zinalenga kudumisha na kukuza utu na heshima ya binadamu.

Ukosefu wa misingi na kanuni za utawala bora ni kati ya mambo yanayochangia kugumisha mchakato wa Uinjilishaji Mpya katika baadhi ya nchi za AMECEA. Afrika ya Mashariki kwa sasa inakabiliwa na vitisho vya vitendo vya kigaidi, misimamo mikali ya kidini pamoja na udani; mambo ambayo yanahatarisha haki, amani na utulivu Sudan, Sudan ya Kusini, Kenya, Somalia na Tanzania. Mashambulizi na mauaji ya kigaidi yanayoendelea kusikika sehemu mbali mbali za Afrika Mashariki na kati yanatishi amani na mustakabali wa maendeleo ya watu: kiroho na kimwili.

Kuna haja kwa viongozi Barani Afrika kuhakikisha kwamba, wanajikita kwa ajili ya kutafuta mafao ya wengi; kusimamia vyema rasilimali ya taifa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wote kwa kuondokana na tabia ya ubinafsi inayojengeka miongoni mwa wananchi wa Bara la Afrika kwa kupenda mno fedha na mali, kiasi cha kutumbukia kwa urahisi katika saratani ya rushwa, ufisadi na wizi wa mali ya umma. Uchu wa madaraka ni tatizo na changamoto inayopaswa kufanyiwa kazi kwa umakini mkubwa, vinginevyo, Bara la Afrika litaendelea kuwa ni uwanja wa fujo.

Kanisa Katoliki Barani Afrika limekuwa likichapisha nyaraka za kichungaji, kwa kutumia Tume ya haki na amani, Ibada na huduma katika taasisi ya elimu ya juu. Mbinu hizi zote bado hazijazaa matunda yanayokusudiwa. Kuna haja kwa Maaskofu wa AMECEA kuibua mbinu mkakati utakaowashirikisha wanataaaluma Wakristo katika kufikisha hoja na utekelezaji wake. Kanisa liendelee kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu na kuzuia kinzani na mipasuko ya kijamii pale inapowezekana!







All the contents on this site are copyrighted ©.