2014-07-19 08:44:58

Muda wa longo longo umekwisha, watu wanataka kuona maendeleo!


Askofu mkuu Gabriel Mbilingi, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM, amewataka Waafrika kutoa maana ya kweli kuhusu maendeleo endelevu yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. RealAudioMP3

Hii ni changamoto iliyotolewa na SECAM wakati wa maadhimisho ya Kongamano la Siku mbili lililofanyika kwenye Chuo Kikuu cha Kipapa cha Urbainiana, kilichoko mjini Roma kwa ajili ya kuwaenzi watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II, ambao wamechagia kwa kiasi kikubwa katika ustawi na maendeleo ya Kanisa Barani Afrika.

Kongamano hili liliongozwa na kauli mbiu Kanisa Barani Afrika: kutoka Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican hadi mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo: mchango wa Papa Yohane XXIII na Yohane Paulo II.

SECAM inasema, kuna haja kwa wananchi wa Bara la Afrika kuhakikisha kwamba, wanatumia rasilimali watu, fedha na vitu katika mchakato wa kujiletea maendeleo yao wenyewe kuliko tabia ya sasa ya kutegemea misaada kutoka ng’ambo hali ambayo inadhalilisha utu na heshima ya wananchi wa Bara la Afrika. Hii inatokana na ukweli kwamba, baadhi ya misaada inayotolewa imekuwa na masharti makubwa ambayo wakati mwingine yanakwenda kinyume cha utu na maadili mema.

Familia ya Mungu Barani Afrika ilitumia fursa ya kuwatangaza watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II kuangalia jinsi ambavyo Kanisa barani Afrika limeendelea kumwilisha Mafundisho ya Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican katika maisha na utume wake. Kanisa Barani Afrika linaendelea kujipanga vyema zaidi ili kuchangia katika ustawi na maendeleo ya Bara la Afrika, kwa kutoa taswira na utambulisho ulio sahihi zaidi, kwa njia ya majadiliano katika jukwaa la imani, tamaduni na maendeleo endelevu.

Kongamano hili la Kimataifa limehudhuriwa na Makardinali, Maaskofu, Mabalozi, wanataalimungu na falsafa kutoka Barani Afrika, Wanafunzi kutoka vyuo vikuu vilivyoko mjini Roma na viunga vyake. Kwa hakika ni Kongamano ambalo lilikuwa limesheheni matumaini ya Familia ya Mungu Barani Afrika.

Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki Cor Unum, katika hotuba yake ya ufunguzi alisikitika kusema kwamba, Familia ya Mungu Barani Afrika inakumbana na na changamoto mbali mbali zinazoibuliwa kutoka katika utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Lakini Bara la Afrika linapaswa kukumbuka kwamba, lina mchango mkubwa katika ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kiulimwengu, dhana inayopaswa kufanyiwa kazi kwa ari na bidii kubwa zaidi. Kardinali Gianfranco Ravasi, Rais wa Baraza la Kipapa la Utamaduni amepongeza uhusiano unaoendelea kujengeka kati ya Baraza lake na SECAM katika kukuza na kudumisha majukwaa ya utamaduni na kwamba, Baraza lake, linataka kuwekeza zaidi katika ustawi wa Kanisa Barani Afrika.

Kwa ufupi mada zilizochambuliwa katika kongamano la siku mbili kama sehemu ya mchakato wa kuwaenzi Watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II zimegusia kuhusu: Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na utekelezaji wake kwa Kanisa Barani Afrika; mchango wa Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na Mapapa waliofuatia na utekelezaji wake na Kanisa Barani Afrika.

Wataalam pia waligusia mwangwi wa kazi zilizofanywa na Chama cha wanataalimungu Barani Afrika, (ATA) kuhusu Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Mchango wa Papa Yohane XXIII na Yohane Paulo II Barani Afrika pamoja na mageuzi yaliyojitokeza Barani Afrika mara tu baada ya maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Imeandaliwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.