2014-07-17 16:10:16

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 16 ya Kipindi cha Mwaka A wa Kanisa


Mpendwa mwana wa Mungu, tunatafakari Neno la Mungu Dominika ya 16 ya mwaka A wa Kanisa. Wewe nami tunaalikwa tena kutambua kuwa huruma ya Mungu ni ya milele na ni kwa ajili ya wadhambi na waliowema. RealAudioMP3

Kamwe Mungu hataweza kumpatiliza awaye yote aombaye huruma yake na kutubu. Tunaambiwa hata kama dhambi za mtu huyu zingekuwa nyekundu kiasi gani, Mwenyezi Mungu atazigeuza na kuwa nyeupe. Hata hivyo yatupasa kutambua pia kuwa Mungu ni mwenye haki, kumbe kama mmoja hataacha njia yake mbaya, mwishoni atakuwa ni chukizo na hivi kutupwa nje ya ufalme wa Mungu.

Mpendwa mwana tafakari, katika somo la kwanza tunaona jinsi mwandishi anavyojaribu kuwaimarisha wana wa Israeli ili kuwatoa katika wasiwasi walionao. Waisraeli wanajiuliza mbona mambo yetu na hasa katika uwanja wa biashara hayafanikiwi? Mbona wapagani wasiomcha Mungu wanafaulu katika shughuli zao? Wana wa Israeli wangependa Mungu awapatilize wapagani wasiomcha Mungu! Ndiyo kusema wale wote wafanyao ubaya hivi leo, wangepaswa kupatilizwa na kupotea kabisa toka uso wa nchi!

Basi tokana na mtizamo huo mwandishi wa somo la kwanza anawajibu na anatujibu sisi hivi leo kuwa Mungu ni upendo mkamilifu ambao haubagui awaye yote badala yake ni kwa ajili ya wema na wabaya. Mungu wetu hawafanyi watu waamini kwa njia ya mabavu bali hujiingiza katika historia ya maisha yao na kuwageuza taratibu, ndiyo kusema Roho wa Mungu, aliye Roho wa upole, mfariji, Roho wa elimu na hekima ya kimungu, hutoa nafasi kwa wadhambi watubu na kisha wamwendee yeye katika uhuru kamili wa wana wa Mungu.

Ujumbe huu unajionesha wazi katika injili ambapo tunaona Mwana wa Mungu anasiha mbegu ya imani na mbele yake kuna wapinzani walioadui wa mbegu hiyo. Je mwana wa Mungu atawapatiliza hawa maadui wa imani? Hapana, daima ana subira kwa ajili yao, akiwajalia Roho wa elimu na hekima ili polepole watubu na kuiacha njia yao mbaya. Hata hivyo kama hawatapokea zawadi hiyo ya toba basi haki ya Mungu hutenda kazi yake.

Mtakatifu Paulo anasisitiza daima kuwa tunapaswa kuomba paji la Roho Mtakatifu ili kuweza kutusaidia kuhuisha sala yetu iliyodhaifu ili ipate uhakika wa kupokelewa na Mungu Baba. Kwa paji la Roho Mtakatifu mwanadamu anageuka kuwa dhabihu safi mbele ya Mungu. Kwa paji la Roho Mtakatifu mwanadamu anaweza kugundua huruma ya Mungu iliyo kuu ambayo huja kama mvua kwa ajili ya wote. Mwanadamu pia ataweza kuona katika Neno la Mungu kuwa Kristo Mkombozi alikuja si kwa ajili ya wema tu bali kwa ajili ya wote.

Mpendwa mwana wa Mungu, Neno la Mungu daima hutualika kukubali tukiwa na utulivu wa moyo uwepo wa dhambi katika ulimwengu. Kukubali uwepo wa dhambi si kukumbatia dhambi bali utambuzi unaosaidia kuanza vita vya kiroho dhidi ya dhambi hiyo. Tunapigana vita tukiwa na uhakika kwamba Kristu ameishinda dhambi na siku moja upendo wa Mungu utafuta yote. Hili latudai unyenyekevu, maisha ya sala na utafiti wa kiinjili tukiulekea msalaba wa Kristu. Tumsifu Yesu Kristu.

Tafakari hii imeletwa kwenu na Padre Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.