2014-07-16 10:35:50

Maaskofu wanawake! Kikwazo katika majadiliano ya kiekumene!


Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza linasema, kitendo cha Kanisa Anglikani kuridhia wazo la kuwaweka wanawake wakfu ili kuwa Maaskofu ni kikwazo kikubwa katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene kati ya Makanisa. Kanisa Katoliki, kwa upande wake litaendeleza mchakato wa majadiliano ya kiekumene kwani hii ni sehemu ya mikakati yake ya kichungaji na kwamba, litaendelea kushirikiana na Kanisa Anglikani kadiri inavyowezekana.

Hivi karibuni, Sinodi ya Kanisa Anglikani iliyokutana tarehe 14 Julai 2014 huko New York, imepitisha na kuridhia wazo la wanawake kuwekwa wakfu kuwa Maaskofu katika Kanisa Anglikani. Dhana hii imekuwa ikifanyiwa kazi na Kanisa Anglikani kwa miaka mingi na imekuwa ni chanzo cha migawanyiko ndani ya Kanisa Anglikani, kwa baadhi ya waamini kutoafiki wanawake kuteuliwa na hatimaye, kuwekwa wakfu kuwa Maaskofu wa Kanisa Anglikani.

Itakumbukwa kwamba, Kanisa Katoliki na Kanisa la Kiorthodox ndiyo bado ambayo hayatoi nafasi kwa wanawake kuteuliwa na hatimaye kuwekwa wakfu kuwa Maaskofu. Kanisa Katoliki limepiga hatua kumbwa katika majadiliano ya kiekumene tangu baada ya maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, kwa kujenga na kuimarisha mshikamano wa kidugu, changamoto kubwa iliyoko mbele ya Makanisa haya wanasema Maaskofu wa Uingereza ni kuendelea kutolea ushuhuda makini wa Injili ya Kristo kwa watu wa nyakati hizi.

Wakati huo huo, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni Dr. Olav Tveit amelipongeza Kanisa Anglikani kwa kufanya maamuzi magumu ya kukubali na hatimaye kuridhia kwamba, wanawake wanaweza kuteuliwa na kuwekwa wakfu kuwa Maaskofu. Hii ni "baraka kwa Kanisa Anglikani". Katika nchi kama Amerika na Ustralia kuna Maaskofu wanawake tangu mwaka 1994, lakini nchini Uingereza wazo hili halikukubaliwa hadi mwaka huu, Sinodi ya Kanisa Anglikani iliporidhia wazo hili.







All the contents on this site are copyrighted ©.