Zaidi ya watu laki moja kutoka katika nchi sabini wanatarajiwa kuhudhuria katika Ibada
ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumtangaza Mtumishi wa Mungu Askofu Alvaro del Portillo,
mwandamizi wa kwanza wa Mtakatifu Josemaria Escrivà de Balaguer katika kuliongoza
Shirika la Kazi ya Mungu, maarufu kama “Opus Dei” kuwa Mwenyeheri.
Ibada itaadhimishwa
katika Jimbo kuu la Madrid, hapo tarehe 27 Septemba 2014. Taarifa hii imetolewa na
kamati ya maandalizi ya kumtangaza Mtumishi wa Mungu del Portillo kuwa Mwenyeheri
sanjari na kalenda ya maadhimisho haya. Itakumbukwa kwamba, Jimbo kuu la Madrid ndipo
mahali alipozaliwa Mtumishi wa Mungu del Potillo, lakini sehemu kubwa ya maisha yake
alikuwa mjini Roma, yaani tangu mwaka 1943 hadi mwaka 1994, alipofikwa na mauti kadiri
ya mpango wa Mungu.
Masalia ya mwili wa Mtumishi wa Mungu del Portillo yamehifadhiwa
kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria Mama wa amani, lililoko mjini Roma. Baada ya maadhimisho
haya hapo tarehe 29 Septemba na tarehe 2 Oktoba, washiriki wengi katika matukio haya
watarejea mjini Roma na kuendelea kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani
kwa kumjalia Mtumishi wake del Portllo kutangazwa kuwa Mwenyeheri, mfano wa kuigwa
katika utakatifu wa maisha!