2014-07-14 10:26:01

Msikate tamaa na kushindwa na ubaya! Endeleeni kusali!


Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya Sala na tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili tarehe 13 Julai 2014 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican aliwaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuungana pamoja naye kwa ajili ya kusali na kuombea amani katika Nchi Takatifu.

Bado anakumbuka lile tukio la tarehe 8 Juni 2014 alipokutana na kusali pamoja na Patriaki Bartolomeo wa kwanza, Rais Peres wa Israeli pamoja na Rais Abbas wa Palestina ili kuombea amani Mashariki ya Kati!

Baba Mtakatifu anasema kwamba, baadhi ya watu wanaweza kufikiri kwamba, mkutano ule wa sala haukuwa na mafanikio yoyote, lakini hii si kweli, kwani Sala inawasaidia waamini kutokatishwa tamaa na kushindwa na ubaya, wala matumizi ya nguvu kushika hatamu badala ya majadiliano na upatanaisho. Baba Mtakatifu anawaalika wadau mbali mbali kuongeza juhudi zao katika kukomesha uadui na chuki kati ya watu, ili amani na mafao ya wengi yaweze kushika mkondo wake.

Baba Mtakatifu amewaongoza waamini na watu wenye mapenzi mema waliokuwa wamefurika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kusali kwa ajili ya kuombea amani, ili Mwenyezi Mungu awaongoze katika amani ya kweli, awajalie ujasiri wa kukataa kishawishi cha vita kwani kwa njia ya vita kila kitu kinapotea, awakirimie ujasiri wa kuonesha kwa vitendo njia za ujenzi wa amani pamoja na kuwawezesha kusikiliza kilio cha wananchi wao wanaotaka wabadilishe silaha kuwa ni vyombo vya amani, wasi wasi na woga kuwa ni alama ya matumaini na kinzani, kuwa ni kielelezo cha msamaha!

Baba Mtakatifu pia aliwakumbusha waamini kwamba, Jumapili iliyopita Mama Kanisa ameadhimisha Siku ya Mabaharia Duniani, kwa kuwataka waamini kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya Mabaharia. Anawaalika wahudumu wa maisha ya kiroho pamoja na watu wa kujitolea kuwasaidia mabaharia na kwamba, anawaweka wote chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria nyota ya bahari.

Amewashukuru viongozi wa Kanisa na waamini wa Familia ya Radio Maria waliokuwa wanafanya hija ya maisha ya kiroho katika madhabahu ya Bikira Maria wa Jasna, Gòra, Czestochowa, Poland. Anawashukuru kwa kumkumbuka na kumwombea katika maisha na utume wake.

Baba Mtakatifu ametambua uwepo wa wanashirika wa Shirika la Mtakatifu Camillo wa Lellis, wanaoadhimisha Jubilee ya miaka 400 tangu alipofariki dunia. Anawaalika wanashirika hawa kuwa kweli ni alama ya Yesu Kristo, Msamaria mwema anayejinyenyekesha kwa ajili ya kuwaganga majeraha ya mwili na roho kwa kuwapaka mafura ya faraja na divai ya matumaini. Anawapongeza kwa huduma makini wanayotoa kwa ajili ya wagonjwa, waendeleze upendo kwa wagonjwa.







All the contents on this site are copyrighted ©.