2014-07-12 10:49:10

Wajumbe wa AMECEA, Karibuni Malawi!


Serikali ya Malawi imesema kwamba, itajitahidi kuhakikisha kwamba, ulinzi na usalama wakati wa maadhimisho ya mkutano mkuu wa kumi na nane wa AMECEA unaimarishwa zaidi, ili kuwawezesha wajumbe kutekeleza dhamana na wajibu wao kwa amani na utulivu. Hayo yameelezwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi baada ya kufanya mkutano na viongozi wa Serikali ya Malawi hivi karibuni.

Serikali ya Malawi imeonesha utayari wa kulisaidia Kanisa katika maadhimisho ya mkutano mkuu wa AMECEA unaofanyika nchini humo, kama kielelezo cha upendo, mshikamano na ukarimu kutoka kwa wananchi wa Malawi kwa ugeni mzito utakaokuwemo nchini humo kuanzia tarehe 14 hadi tarehe 27 Julai 2014 huko Lilongwe.

Ujumbe kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi umepata pia fursa ya kukutana na kuzungumza na Makamu wa Rais wa Malawi Bwana Saulos Chilima, aliyehabarishwa kuhusu kamati mbali mbali zilizoundwa ili kurahisisha maadhimisho ya AMECEA huko Malawi. Professa Peter Arthur Mutharika, Rais wa Malawi anafuatilia tukio hili kwa ukaribu zaidi na anatarajiwa kuhudhuria katika Ibada ya ufunguzi wa mkutano mkuu wa AMECEA hapo tarehe 17 Julai 2014 pamoja na kuwahutubia wajumbe wa mkutano huo.







All the contents on this site are copyrighted ©.