2014-07-10 08:49:05

Dumisheni misingi ya ndoa na familia, epukeni "michepuko"


Wajumbe kutoka Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA, walishiriki katika kongamano kuhusu changamoto zinazoikabilia familia katika karne ya ishirini na moja mintarafu utandawazi katika mazingira ya Kiafrika. RealAudioMP3

Kongamano hili ni sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia itakayoadhimishwa mjini Vatican kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba 2014. Wajumbe wanakiri kwamba, kuna mabadiliko makubwa yanayoendelea kujionesha katika familia ya mwanadamu. Kongamano hili limefanyika kwenye Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Afrika Mashariki na Kati, CUEA na kwamba, wajumbe wamesisitizia umuhimu wa Vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki kuanza kuangalia uwezekano wa kutoa kozi maalum kwa ajili ya maisha ya ndoa na familia.

Lengo ni kuwajengea wanandoa pamoja na wanandoa watarajiwa uelewa mpana wa maisha haya tangu awali, kuliko kusubiri mafunzo ya ndoa, wiki mbili kabla ya kufunga Ndoa Takatifu ambayo ina dumu hadi pale kifo kitakapowatenganisha. Kumbe, ni muhimu wanandoa wakajiaandaa barabara na wala si kukurupuka tu, kwa sababu ya mambo mpito kama vile: fedha, cheo au nafasi ya mtu! Hapa Waswahili wanasema, wakati mwingine, hapendwi mtu, ila pochi tu!

Jamii inajengwa katika msingi wa ndoa ndiyo maana Kanisa linaendelea kusimama kidete kulinda na kutetea misingi bora ya maisha ya ndoa na familia inayojengeka katika upendo wa dhati kati ya Bwana na Bibi, kadiri ya mpango wa Mungu, yaani kuzaa na kuongezeka ili wapate kuijaza dunia. Haitoshi tu kuzaa na kuondoka, kwani watoto wanahitaji matunzo na malezi bora kutoka kwa wazazi wao.

Kumbe, wazazi wanapaswa kuwajibika barabara katika malezi na makuzi ya watoto wao: kiroho na kimwili, ili hatimaye, waweze kuwa na uwezo wa kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika hija ya maisha yao hapa duniani. Licha ya changamoto kubwa zinazoikabilia Familia ya binadamu, kuna haja ya kupambanua mambo msingi yanayogusa utu na heshima ya binadamu na haya yanapaswa kuvaliwa njuga, hadi kieleweke!

Mabingwa mbali mbali katika masuala ya ndoa na familia wameshirikisha mang’amuzi na ufahamu wao, tayari kuona familia Barani Afrika zinaendelea kujikita katika tunu bora za maisha badala ya kuiga mambo hata yale ambayo kweli ni kinyume cha tunu msingi za maisha ya Kikristo na Kiafrika.

Pamoja na mambo mengine, wajumbe pia wamepembua Waraka wa Papa Francisko, “Evangelii gaudium” Injili ya Furaha kadiri ya mazingira ya Bara la Afrika. Wamekazia dhamana na wajibu wa wazazi na walezi katika kuwafunda watoto, kwani Waswahili husema, samaki mkunje angali mbichi, akikauka, hapo utapata shida.

Lakini, ikumbukwe kwamba, Kanisa Barani Afrika lina dhamana ya malezi kwa watoto wake, kumbe, katekesi makini inahitajika na majiundo endelevu ni muhimu kwa waamini walei ili kuwajengea uwezo wa kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha.

Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wajitaabishe kusoma Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki ambao kweli ni muhtasari wa Imani, Sakramenti za Kanisa, Maisha Adili pamoja na Sala. Waamini wakiifahamu vyema Katekisimu na kuimwilisha katika maisha na vipaumbele vyao, kweli wanaweza kuwa ni chachu na mwanga wa dunia katika mchakato wa kuyachachua malimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha.

Wajumbe wanasema, kuna uhusiano wa karibu kati ya Familia na Maendeleo endelevu ya binadamu: kiroho na kimwili. Familia nyingi zinakumbana na changamoto nyingi za maisha ya kijamii na kiuchumi, kiasi kwamba, wakati mwingine zinabaki njia panda. Njia za mawasiliano ya jamii zinaendelea kupewa nafasi ya pekee katika majiundo ya maisha ya kifamilia.

Kwa upande wa Bara la Afrika, njia za mawasiliano ya jamii ni upanga wenye makali kuwili mikononi mwa binadamu, zinaweza kusaidia familia, lakini kama watu hawatakuwa makini, njia hizi na mitandao ya kijamii zinaweza kuwa ndo mwanzo wa kukengeuka kwa familia nyingi.

Barani Afrika bado ndoa mchanganyiko zinaendelea kushamiri kwani mapenzi ni chaguo la mtu. Hapa kuna haja ya kuwasaidia Wakristo wanaofunga ndoa mchanganyiko katika kutekeleza majukumu ya malezi kwa watoto wao, jambo ambalo kimsingi si rahisi sana kwa watu wengi, hasa ukizingatia mfumo dume unaoendelea kutawala Barani Afrika.

Wajumbe wamekiri kwamba, kuna haja ya kufanya uwiano mzuri kati ya kazi na maisha ya kifamilia. Kuna baadhi ya watu wamejikuta wakizama kwenye kazi kiasi cha kudhoofisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia na matokeo yake, uaminifu, ukweli na udumifu vinawekwa rehani, hapa ni mwanzo wa kuchuma majanga kama vile Ukimwi, Magomvi ndani ya nyumba na talaka!








All the contents on this site are copyrighted ©.