2014-07-09 11:38:51

Achana na kabumbu! Utalala mlango wazi!


Mashindano ya kombe la dunia kwa mwaka 2014 huko Brazil, ni tukio ambalo limevuta hisia za watu wengi pamoja na kuonesha mshikamano wa dhati na timu pamoja na wachezaji wenyewe. Watu wamerukaruka kwa furaha kama Kulungu, timu zao ziliposhinda; wamelia na kuombolezwa pale walipochakazwa kwa mabao utadhani ni mpira wa pete!

Watu wamekesha ili kufuatlia na kuangalia hatima ya kabumbu ilivyokuwa inatandazwa huko Brazil, kwa hakika kuna mengi ya kuweza kujifunza katika kipindi chote cha mashindano ya Kombe la Dunia kwa Mwaka 2014.

Baraza la Maaskofu Katoliki Chile linawaalika waamini kutafakari kwa kina baadhi ya tunu msingi za maisha ya Kikristo kwa kung'amua umuhimu wa kujenga na kuimarisha mshikamano wa kidugu kati ya waamini na Jamii katika ujumla wake. Waamini wajenge na kuimarisha utamaduni wa kukutana ili kushirikishana mang'amuzi mbali mbali ya maisha ya kiroho, kiutu na kijamii. Ari, moyo na ushabiki ambao watu wameonesha kwa timu zao za kitaifa, unaoweza pia kuwasaidia waamini kujenga uhusiano wa karibu na Yesu pamoja na kuipenda Injili, kiasi hata cha kuweza kuwa tayari kuitolea ushuhuda makini katika uhalisia wa maisha!

Baraza la Maaskofu Katoliki Chile linawataka waamini kujenga utamaduni wa kukutana ili kushirikisha tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili, tayari kujitosa kimasomaso kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake; ili kuonesha uwepo wa Mungu kati ya watu wake. Hapa jambo linalopewa kipaumbele cha pekee ni umoja, upendo na mshikamano wa kidugu kama timu ya mpira pasi na ubinafsi. Ni changamoto ya kuwaangalia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Waamini wajifunze kujisadaka kwa ajili ya kushiriki katika maisha na utume wa Kanisa katika utekelezaji wa mikakati ya kichungaji; waamini wajenge na kuimarisha upendo na mshikamano wa dhati katika mambo msingi ya maisha; umoja na udugu viwe ni nguzo kuu katika maisha na utume wa Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.