2014-07-08 12:25:25

Jubilee ya miaka 50 ya Uhuru wa Malawi!


Professa Arthur Peter Mutharika, Rais wa Malawi, Jumapili iliyopita amewaongoza wananchi wa Malawi katika kilele cha maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 tangu Malawi ilipojipatia uhuru wake kutoka kwa Mwingereza. Katika kipindi hiki, Malawi imepata mafanikio makubwa katika sekta ya elimu, afya pamoja na miundo mbinu. Hali ya maisha ya wananchi wa Malawi imeboreka maradufu na kwamba, demokrasia imekuwa na kuongezeka, sasa Malawi ni kisiwa cha amani Barani Afrika.

Hayo yamesemwa na Rais Mutharika katika hotuba ya maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya uhuru wa Malawi iliyohudhuriwa na viongozi mbali mbali kutoka katika Nchi za SADC. Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe ameipongeza Malawi kwa kuonesha ukomavu wa kisiasa na demokrasia pamoja na kuendeleza mchakato wa mageuzi ya kisiasa, kiuchumi na kijamii kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Malawi.

Katika maadhimisho haya, Serikali ya Malawi imetoa msamaha kwa wafungwa 403 kama kielelezo cha kusherehekea Jubilee ambayo kimsingi ni alama ya shukrani kwa Mwenyezi Mungu. Malawi imeendelea kufanya mageuzi ya viongozi wa Serikali kwa njia ya demokrasia na hivyo kuwa ni kati ya nchi zinazodumisha amani Barani Afrika anasema rais Athur Mutharika.







All the contents on this site are copyrighted ©.