2014-07-05 13:30:49

Maisha ya mtu mkimbizi.....


Makala Dunia Mama, yanaendelea kwa mfululizo, kutafakari maisha mchanganyiko katika jamiiya leo, kwenye ulimwengu wa utandawazi. Leo na tutazame kwa makini maisha ya mtu mkimbizi. Je mkimbizi ni nani hasa? Na kwa nini awepo ? Je kuna manufaa yoyote ya kuwa mkimbizi? Na jamii ifanye nini kuepusha janga la ukimbizi ?

Maana ya "Mkimbizi" inaweza kutofautiana, lakini wengi wanakubaliana kwamba, mkimbizi ni mtu anaye toka katika nchi yake kwa kushurutishwa na hali fulani inayotishia maisha yake, mara nyingi ikitokana na vita, mateso ya kidini au mateso ya kisiasa. Ufafanuzi Umoja wa Mataifa kwa wakimbizi ni "mtu yeyote ambaye: kutokana na hofu ya kuteswa kwa sababu ya rangi, dini, utaifa, uanachama wa kikundi fulani cha kijamii, au maoni ya kisiasa, huondoka nchini mwake na kwenda nje ya nchi yake mara nyingi bila idhini au kwa kutoroka kwa kuwa hawawezi au, kutokana na hofu kuomba ulinzi wa nchi hiyo. Hivyo kuna makundi au aina nyingi za wakimbizi , wakimbizi wa njaa, vita, jamii ,kidini ,kisiasa ,ubaguzi wa rangi, Kundi la kijamii, Wale walio katika hofu ya mateso hasa wanawake na watoto.


Sheria za kimataifa za wakimbizi zinamtaja mkimbizi kama mtu ambaye anatafuta hifadhi salama katika nchi za kigeni kwa sababu ya vita na vurugu, au nje ya hofu ya mateso, katika nchi yake. . Pia kuna wale wanaokimbia maeneo yao na kwenda katika eneo jingine mahali palipo salama zaidi kwa maisha yao, nao pia Umoja wa Mataifa unawatambua kuwa ni wakimbizi.

Kwa kifupi, kuna wakimbizi wa njaa, ambao wanatoka katika maeneo yao na kuhamia katika maeneo mengine kutokana na ukosefu mkali wa chakula hivyo wanahama kwa ajili ya kusalimisha maisha yao ili wasife njaa. Na wakimbizi wa dini ,ni wale wanaokimbia madhulumu ya kunyimwa haki ya kufuata imani yao kama inavyotakiwa, mara nyingi wakinywa haki hii kwa vitisho hata vya kuuawa, na mara nyingi watu huwa ni kundi dogo kati ya kundi kubwa la imani moja , kama inavyo sikika sasa katika mataifa kama Pakistan, Libya, Sudan Somalia, Wakristo wanaishi kwa hofu kubwa na wengi wao wanakimbilia sehemu zingine zenye usalama zaidi. Aidha kuna wakimbizi wa kiuchumi, hawa hukimbia hali ngumu ya maisha nakwenda katika nchi nyingine wanakofikiri wanaweza kuboresha hali ya maisha yao. Mara nyingi wakimbizi hawa wa uchumi huondoka nchini mwake kwa kujiandaa taratibu si sawa na mkimbizi wa vita, au mkimbizi wa mateso, ambaye huutumia mwanya wowote unaopatikana kuondoka bila maandalizi. Lakini makundi yote haya huwa na tabia moja inayofanana, kuondoka mahali wanapotakiwa kuwa na kuhamia maeneo mengine bila idhini rasmi. Ni watu wanaotoroka toka makwao na kuingia katika maeneo mapya , kutokana na moja ya sababu zilizotajwa hapo juu.

Leo hii tunapata habari nyingi mbalimbali juu ya wakimbizi . Habari za wakimbizi wanao kufa maji wakijaribu kuvuka bahari kinyume cha sheria, wakimbizi wanaokufa kwa njaa jangwani wakikimbia njaa, umaskini au maonevu katika nchi zao, wakimbizi wanaokimbia madhulumu ya nyumbani hasa wanawake na watoto, wakimbizi wa vita n. . Ni habari za kusikitisha na kutisha , zenye kuipenya mioyo ya watu wenye mapenzi mema, kama Papa Francisko alivyoeleza wakati alipokitembekea kituo cha wakimbizi cha Lampedusa Italia, Julay 8, 2013. Kituo cha Lampedusa ambacho kimekuwa mlango maarufu wenye kupokea maelfu ya wakimbizi, wanaojaribu kuingia bara la Ulaya tokea Afrika na mataifa mengine ya Ulaya na Asia Mashariki.

Kwa mujibu wa takwimu za UNHCR, leo hii duniani kuna jumla ya watu zaidi ya milioni 43 wanaoishi kama wakimbizi mahali fulani, wale waliobaki ndani ya nchi zao na wale walio hamia nchi nyingine bila kibali. Na kwa mujibu wa shirika la Mpango wa Mpango wa Chakula Duniani (WFP) , shirika lenye kutoa hutoa msaada wa chakula kwa wakimbizi, Afrika ina wakimbizi milioni 2.4. Wanaishi katika makambi ya 200 yaliyo tawanyika katika nchi 22, wengi wa wakimbizi hawa ni waathirika wa vita na mateso.
Shirika kwa ajili ya Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR kwa kushirikiana na mashirika mengine yanayo wajibika na utoaji wa misaada ya kibinadamu kama WFP, Caritas, UNICEF, kwa makundi ya watu walio katika mahangaiko na mateso e, huufanya kila jitihada za kuwasiliana na jumuiya ya kimataifa kupata fedha za kulisha wakimbizi hao. Bahati mbaya mara kwa mara hukabiliwa na uhaba wa fedha kukidhi mahitaji msingi ya kibinadamu kwa wakimbizi, wakati mwingine hulazimika hata kupunguza mgawo wa chakula, kama ilivyo sasa, UNHCR, imelazimika kupunguza mgao wa chakula kwa watu 450,000 wanaoishi makambini katika Jamhuri ya Afrika ya Kati, Chad na Sudan ya Kusini kutokana na uhaba wa chakula. Na pia zaidi ya wakimbizi 338,000 eneo la Liberia, Burkina Faso, Msumbiji, Ghana, Mauritania na Uganda, pia wanapokea chini ya nusu asilimia 50 ya misaada wa chakula.


Mkurugenzi wa Mpango wa Chakula (WFP), katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Bwana Ohlsen, katika mahojiano na Redio Vatican hivi karibuni alieleza kuwa , kila mkimbizi hutumia dola 1.5, katika gharama za msaada wa msaada wa chakula na mahitaji yake mengine ya kila siku. Hivyo kutokana na hali hiyo, kila mkimbizi hupata mlo mmoja tu kwa siku, ambao si wa kushibisha inavyotakiwa. . Hivyo hii ina maana watu hawa hasa vijana na watoto wanaotazamiwa kuwa watu wazima wa baadaye ambao miili yao inahitaji lishe bora kuijenga miili sasa miili hiyo inanyong’onyezwa na ukosefu wa lishe bora. Katika hatua hii, wengi wana dalili wazi kama vile matumbo kuvimba, udhaifu wa mwili unaojitokeza kama uvivu, kutopenda kazi, kuwa watu wa hasira, kuchanganyikiwa, mfadhaiko na kushikwa na maradhi kwa urahisi.
Kwenye hali hii ngumu ya kimaisha baadhi ya wakimbizi huamua kuondoka kambini kisirisiri na kujichanganya na jamii iliyo karibu nao, wengine hawa wanawake hujiingiza katika ukahaba, au kutumikishwa kama mtumwa na hasa watoto, au kusajiliwa kama askari, hasa watoto na katika matukio mengine ya kutisha, ili mradi tu aweze kupata chochote za kijikimu kimaisha.

Kwa upande mwingine, kuna wakimbizi wanao endelea kutunza hadhi yao , na hivyo huwa tayari kushirikiana na utawala mahalia walimo kimbilia, wakiwa tayari kuzalisha chakula chao, wakati wanasubiri utulivu urejee katika sehemu zao . Mkimbizi mmoja katika kituo cha Lampendusa , alimshuhudia Papa Francisco matatizo yao kwamba, wamekimbia kutoka nchi zao kwa sababu mbili kwanza ni saba bu za kisiasa na pili ni hali mbaya ya uchumi. Na hivyo walikuwa na hamu kubwa ya kupata mahali penye utulivu, ili waweze pia kushiriki katika harakati za kijamii na kujiinua kiuchumi. Lakini katika harakati hizi pia kuna vikwazo na matatizo mengi kuliko walivyotazamia. Na wala hawawezi kurudi katika nchi zao kwa kuwa wataonekana kuwa wasaliti na hivyo heri kupambana mateso yaliyo mbele yao.

Baba Mtakatifu Francisco kwa huruma na upendo aliwatazama watu hao na kuwaambia jinsi moyo wake unavyogusa na habari za watu wanaokufa wakiwa katika harakati za kutaka kuokoa maisha yao. Katika hotuba yake aliwathibitishia wote bila kujali imani yao kwamba Kanisa liko karibu na kila mmoja wa mtu anayetafuta kulinda na kutetea hadhi ya maisha yake na familia pia .

Baba Mtakatifu alieleza na kutahadharisha kwamba, kila mmoja wetu anaweza kuwa mkimbizi wakati wowote , pale panapotokea maisha kutaka kudhulumika , kama ilivyokuwa kwa familia takatifu , ilikimbilia Misri kusalimisha maisha ya mtoto Yesu aliye taka kuangamizwa na Mfalme Herode.

Baba Mtakatifu Francisco , alimtaka kila mmoja wetu kujihoji , kuna furaha gani hasa kusababisha mateso na dhuluma kwa ndugu yako au jirani yako, au mtu mwingine baki. Kwa nini kutaka kutoa roho ya mwenzako ambayo huwezi kuiumba? Je wanufaika na nini unapomwanga damu ya umwagaji wa damu yako. Papa aliendelea kusema, Mungu anauliza wote wanaofanya madhulumu haya, Je i wapi damu ya ndugu yako anayekulilia. Ni aibu kwamba leo hii duniani hakuna anayejisikia kuwajibika , wote tumepoteza hisia za uwajibikaji kwa mtu mwingine, wawe wanawake au wanaume. Wote tumeanguka katika kundi la unafiki wa Mafarisayo , kama Yesu alivyoeleza katika mfano wa Msamaria mwema . Tunawaona ndugu zetu wake kwa waume wakiwa wametupwa pembezoni mwa barabara , na pengine twawapita tukisema, maskini huyu, na tunaendelea na safari zetu bila kujali. Papa alionya pole hiyo ya maneno unayoitoa bila kumwinamia mtu huyo na kusaidia inakuwa ni unafiki mkubwa. Ni ukwepaji wa wajibu na utamaduni wa kuwajali wengine.

Papa Francisco, tangu mwanzo wa utawala wake, hotuba zake zimeonyesha kujali sana watu masikini na wateswa. Daima anatoa wito kwa kila Mkristu na watu wote Mwenye mapenzi mema kuwa na kujikita katika utamaduni wa kujali na kuwafariji wengine , utamaduni wa kujiweka katika kiatu cha mteswa na kuona jinsi makali ya uchungu wa mateso anamopita mtu huyo .

Katika waraka wake wa Kitume juu ya Injili ya Furaha , kipengere cha tatu, anasema Kanisa ni wazi, lenye kukaribisha kila mtu na limejaa huruma. Kanisa ni sehemu ya huruma, wala si hukumu, kwa sababu Mungu kamwe hachoki kusamehe. Na milango yake i wazi kwa watu wote, si kwa mahitaji si kiroho tu lakini pia hupenda kugawana lilicho nacho kwa wahitaji wengine...

Ingawa ni kweli kwamba, pia kuna ndugu zetu wengi wanaoishi bila urafiki na Yesu. Wengi wanaouona Ukristo kama adui. Pamoja na hatari hizo zote Kanisa litaendelea kutangaza habari njema ya upendo na sifa chanya ya ukarimu, heshima, huruma na uvumilivu katika uchovu wa safari inayoelekea kwenye ukomavu wa upendo. Ni kutangaza habari inayo fungua minyororo yote ya chuki, fitina, wivu, na dhamiri mbaya kwa watu wengine.

Hasa, Papa Francisco amebainisha kuwa, katika umri hii ya upendo, inakuwa kigezo muhimu katika kujenga uhusiano wetu na Waislamu. Amezitaka nchi za mapokeo ya Kiislamu ili kuhakikisha uhuru wa dini kwa Wakristo, kama Waislamu wanavyo furahia uhuru katika nchi za Magharibi. Na ameasa dhidi ya jaribio la kubinafsisha dini, akisema, ni kuhatarisha hali ya usalama na utulivu kwa makundi madogo madogo yanayoonekana kuwa pinzani kiimani, Na makundi yasiyo amini hayapaswi kuweka mikakati ya kunyamazisha imani ya waumini, iwe ni wengi au wachache.

Mafundisho haya ya Papa yanalenga kufuta sababu zote zinazoweza kumfanya mtu kukimbia sehemu yake au nchi na kwenda kutafuta na hali palipo salama. Mama Kanisa anaamini, kuishi pamoja kama ndugu licha ya tofauti za imani na itikadi za kisiasa, unakuwa ni uwanja mzuri wa mmoja kujifunza mengi kutoka kwa mwingine , ni kujitajirisha katika maelewano na urafiki miongoni mwa jamii. Ni kila mmoja kuwa mnyenyekevu wa kumsikiliza mwingine na kujibu kwa heshima. Njia ya majadiliano ni ufunguo wa maisha bora. Lugha chafu, vitisho na utumiaji wa silaha si jawabu katika ufanikishaji wa maisha bora, bali hujenga utengano wenye kuyadhalilisha maisha. Matokeo yake ni uwepo wa watu wanaozikimbia nchi zao.

Baba Mtakatifu anagusa moyo ya matatizo ambayo hugusa maisha ya wanaume na wanawake wa leo na ambayo yana hitaji zaidi uwepo wa Kanisa halisi. Ni lazima Injili imfikie kila mtu, bila ubaguzi kwa lengo la kujenga amani na utulivu duniani. Papa Francisco, alionya dhidi ya watu kubaki bila msimamo thabiti. Tunapaswa , kujenga urafiki na majirani iwe matajiri, au masikini, wagonjwa, wale ambao ni mara nyingi hupuuzwa na kusahauliwa na jamii, watu wanaohangaika kuyaokoa maisha yao, kama ilivyo kwa watu wakimbizi. Ni kuwa pamoja nao katika mashaka yao yote na kuwaimarisha kwa matumaini yaliyosimikwa katika upendo wa Injili(Evangelii Gaudium).
Makala huandaliwa nami TJ Mhella.







All the contents on this site are copyrighted ©.