2014-07-04 08:48:21

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 14 ya Kipindi cha Mwaka A wa Kanisa


Wapendwa wana wa Mungu, tunatafakari Neno la Mungu Dominika ya 14 ya Mwaka A wa Kanisa Ujumbe wa leo: Mungu anajifunua kwa walio maskini, yaani waliotayari kupokea neema na baraka zake. Tukumbuke maneno ya Bwana wetu Yesu Kristo katika Injili ya Luka yasemayo “Roho wa Bwana yu juu yangu kwani ameniweka wakfu niwaletee maskini habari njema” Lk 4:18. RealAudioMP3

Ujumbe huu unajionesha wazi katika mahubiri ya nabii Zakaria kwa taifa la Waisraeli. Wako katika utawala wa kikoloni, wamekata tamaa kwa sababu ya mateso, mashaka na manyanyaso, hawaoni njia ya kutoka katika taabu hiyo. Nabii Zakaria mjumbe wa Mungu anatumwa kuwapelekea habari njema ya furaha, akisema furahi sana Ee binti Sayuni, piga kelele Ee binti Yerusalemu, tazama mfalme wako anakuja…na hivi mwisho wa taabu umefika. Anawatangazia ujio wa Masiha mfalme wa amani atakayewaondoa katika taabu yao.

Katika tangazo hilo la amani anawatahadharisha kuwa mfalme ajaye si wa mabavu wala wa majeshi ya nguvu bali atakuja akiwa amepanda mwanapunda alama ya amani na ya upole. Ni mfalme mnyenyekevu, mtulivu atakayeishi chini ya sheria ili aishinde sheria kwa ndani. Uaguzi huu unakamilika katika Yesu Kristu Mwana wa Mungu anayekubali kuteswa na kuonewa lakini akielekea Yerusalemu mpya.

Mwinjili Matayo anatuonesha mfalme huyu wa amani aliyeaguliwa na nabii Zakaria akisali na kumshukuru Mungu Baba kwa kutimiza mpango wake wa ukombozi kwa ajili ya maskini. Anasali sala ya shukrani ikiwa ni alama mojawapo ya unyenyekevu, kifungo cha mapendo kati ya Mungu Baba na Mwana. Anafanya mawasiliano na Baba yake akituonesha nasi kutolea shukrani kwa Mungu daima kwa njia ya sala na majitoleo mengine mbalimbali katika maisha yetu hapa duniani.

Baada ya kutolea sala ya shukrani anapiga tena hatua nyingine akitufundisha namna ya kumjua Mungu wa kweli. Anasema ili kumjua Mungu Baba njia pekee ni kumjua Mwana aliye mkombozi wa kweli. Kanisa linasadiki kina na linafundisha pasipo mashaka juu ya fundisho hili la Kristu. Wapendwa waamini taifa la Mungu, ujuzi kamili juu ya Mungu uko katikaYesu Kristu aliyeshuka na kupaa Mbinguni. Kristu anafundisha hili akikataa mawazo ya waandishi na walimu wa sheria waliowakandamiza watu na kufikiri kwamba wao ndio pekee wanaoweza kufundisha ujuzi wa kimungu kwa maskini.

Wapendwa, habari njema ya Yesu Kristu, hatuwezi kuiishi na kuishika kina bila msaada wa Roho Mtakatifu. Mtakatifu Paulo akitambua udhaifu wa miili ya kibinadamu anafundisha wazi kuwa miili yetu iliyo na tabia ya kufa inahitaji kuhuishwa na Roho Mtakatifu ili iwe miili ya ufufuko. Kwa nguvu ya Roho tuliyempokea kwa njia ya Sakramenti msingi tunapata nguvu ya kupokea fundisho la Bwana juu ya kumjua Mungu Baba na kufuata sheria na maagizo yake.

Wapendwa taifa la Mungu tumalizie tafakari yetu nikisema kuweni watu wa sala, sala iliyo kiunganishi cha mapendo kati yetu na Mungu katika Utatu Mtakatifu. Tumsifu Yesu Kristu.

Tafakari hii yaja kwenu toka kwa Padre Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.