2014-07-04 08:50:32

"Mungu hachoki kusamehe"


Askofu mkuu Giancarlo Maria Bregantini wa Jimbo kuu la Campobasso-Bojano, Italia anasema kauli mbiu inayoongoza hija ya Baba Mtakatifu Francisko mkoani Molise, Jumamosi tarehe 5 Julai 2014 ni “Mungu hachoki kusamehe”. Akiwa katika majimbo mawili, Kusini mwa Italia, Baba Mtakatifu anatarajiwa kukutana na wafanyakazi, wananchi, wagonjwa, vijana, wafungwa na maskini.

Maandalizi yote yamekamilika. Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanaendelea kumsubiri Baba Mtakatifu Franciko ili kumwonesha upendo na ukarimu wao. Majimbo haya mawili, yanamwomba Baba Mtakatifu Francisko, kwanza kabisa kuwaimarisha katika imani ili waweze kuonja huruma ya Mungu.

Pili, awaombee waamini na watu wenye mapenzi mema ili waweze kujenga utamaduni wa kukutana, ili kukuza matumaini zaidi. Tatu: wanamwomba Baba Mtakatifu awaombee ili waweze kuwa kweli ni watu wanaojikita katika fadhila ya upendo kwa Mungu na jirani, kwa kumthamini na kumjali kila mtu, kwani ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Mambo haya makuu matatu yamekuwepo kwenye sala ambayo waamini wa majimbo haya mawili wamekuwa wakisali tangu Baba Mtakatifu Francisko alipoonesha nia na utashi wa kuwatembelea na kwamba, kauli mbiu inayoongoza hija ya hii ya kichungaji kusini mwa Italia ni “Mungu hachoki kusamehe”. Wananchi wanataka kusikiliza Baba Mtakatifu Francisko atawaambia nini wafanyakazi wanaoendelea kuathirika kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Wananchi wanakabiliwa na ukosefu wa fursa za ajira kiasi cha kuwafanya watu wengi kukosa matumaini ya kesho iliyo bora zaidi na kwamba, utu na heshima yao kama binadamu iko mashakani. Waamini wanamwomba Mwenyezi Mungu ili aweze kuwaonesha njia ya kufuata kwa ajili ya vijana ambao wanaonekana kukosa dira na mwelekeo wa maisha, kama ilivyo kwa vijana wengi duniani kwa sasa!

Askofu Camillo Cibotti wa Jimbo Katoliki Isernia-Venafro anasema, tukio kubwa linalotarajiwa kutekelezwa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa hija yake ya kichungaji ni kutangaza Mwaka wa Jubilee wa Papa Celestini, tangu kuzaliwa kwake kunako mwaka 1215. Mwaliko wa jumla ni kuonesha mshikamano wa upendo na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu. Kimsingi mwanadamu anapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika mikakati ya kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Baba Mtakatifu Francisko anatembelea Jimbo Katoliki la Isernia ambako tarehe 5 Julai 1294 Papa Celestini alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki, hapa kuwa ni sherehe kubwa kwa Jimbo zima kwani mtoto wao alikuwa amechaguliwa kuwa Papa.








All the contents on this site are copyrighted ©.