2014-07-04 15:57:08

Kimbembe mtupu!


Yesu alipoanza maisha yake ya hadharani baada ya miaka yapata thelathini hivi ya umri, alihama toka nyumbani kwake Nazareti akaenda kukaa sehemu inayoitwa Kafarnaum, kando ya ziwa la Galilea na hakurudi tena Nazareti. Hoja kuu za kuhama Nazareti zilisababishwa na wakazi wake.

Hao walikuwa watu wa kufuata mno mila na desturi, yaani, hawakuwa tayari kupokea mabadiliko katika maisha hata baada ya kuona ishara za nyakati zinazodai kufanya mageuzi ya maisha. Huko Kafarnaum kwa mwanzoni mambo yalimwendea vizuri, yaani watu walimpokea kwa hamasa kubwa, lakini ilikuwa kama wasemavyo wahenga “mbuzi mgeni wachungaji wengi”.

Baada ya kupita kitambo kifupi hata huko nako kukaanza kujitokeza mizengwe. Upepo wa mbisho ukamgeukia Yesu kiasi cha kupoteza wafuasi wake wengi: “Kwa ajili ya hayo wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma” (Yoh 6:66).

Mbaya zaidi hata ndugu zake kabisa wa ukoo, akiwamo Mama yake mzazi walisafiri toka Nazareti hadi Kafarnaum kuja kumchukua wakidhani amechanganyikiwa. “Wakaja mamaye na nduguze; wakasimama nje, wakatuma mtu kumwita. Na makutano walikuwa wameketi, wakimzunguka; wakamwambia, “Tazama, mama yako na ndugu zako wako nje, wanakutafuta.” (Mk 3:31-32).

Hoja ni kwamba, hata huko Kafarnao, lugha na mapendekezo aliyotoa kwenye heri nane ilikuwa ngumu kwa watu kupokea na kufuata. Ingawaje kulikuwa na mafanikio ya hapa na pale yaliyotokana na hotuba zake na miujiza kadhaa aliyofanya huko, lakini mwitiko hasi wa watu ulimchanganya Yesu na akawa haelewi kwa nini hawampokei kirahisi.

Kutokana na hali hii, wakati mwingine ilimlazimu kuikaripia miji mbalimbali alimoisha hubiri na kufanya miujiza, na wasikilizaji wake walibaki hamnazo kama walioziba masikio. Yaani watu hawakubadilika katika fikra na hawakuonesha kuongoka. Katika miji wanamokaa watu aina hiyo hakuchelea kuiambia ukweli: “Ole wako Korazini, Ole wako Betsaida” (Mt 11:21). Ole hii, haikuwa na maana ya kulaani, bali ilikuwa ni ya tahadhari ambayo mmoja anapaswa kuwa nayo mbele ya maisha, hasahasa mbele ya kifo. Ni kama vile alitaka kuwaambia: “Jamani tafadhali jihadhalini!”

Katika hayo yote swali nyeti alilokuwa anajihoji Yesu ambalo hata sisi tungeweza kujiuliza ni hili: “Kwa sababu gani hali iko hivyo.” Yaani baada ya Yesu kujitoa nguvu zake zote kufundisha, kuhubiri, kuponya nk, matokeo yake ni kukataliwa, na watu kutokujali chochote wala kubadilika, tungeweza kusema: “wanamshiti.” Kibinadamu mambo yanapoenda kinyume na mategemeo yako, mtu unaweza ukakata tamaa kwani huoni mafanikio ya juhudi na nia zako njema.

Hali kama hii yaweza kumtokea kila mmoja wetu, hususani mzazi, mwalimu au hata kwa kiongozi yeyote yule, anayejitoa nguvu zake zote kuwasaidia wenzake, kuwafundisha, kuwalea, kuwahangaikia kwa namna yeyote iwayo, lakini matokeo yake yanakuwa ni kukataliwa, kuchukiwa na pengine hata kushtakiwa. Hapo mtu unabaki kujihoji bila kupata jibu, kulikoni! na hujui ufanye nini katika hali kama hiyo. Njia wanayotumia wengi ni kuyakimbia mazingira hayo kwa muda na kwenda likizo, au kwenda kujiburudisha kwa namna yoyote ile, na kama hayawezekani kuyatoroka mazingira unabaki kukata tamaa na wengine huamua hata kujinyonga.

Hebu tuone jinsi Yesu anavyoikabili hali hiyo, yaani mambo yanapomwendea kombo. Kwanza kabisa Yesu anazisoma kwanza ishara za nyakati. Namna anavyosoma mazingira ni tofauti na tufanyavyo sisi. Baada ya kuona mwenendo wa mambo unavyoenda, mbinu anayochukua Yesu ni kwenda pahala pa mficho peke yake na kusali.

Lengo la kwenda pahala pa pekee na kusali ni kutaka kuangalia katika mwanga wa kioo ambacho ni Mungu Baba yake, ili katika mwanga huo aweze kuisoma vizuri zaidi ishara hizo za nyakati na kuelewa maana halisi ya matatizo yanayomtokea. Sala siyo kwa ajili ya kupata neema fulani, au kwa ajili ya kumshawishi Mungu akutendee jambo fulani kadiri unavyotaka wewe, la hasha, bali Yesu alitaka aone katika mwanga wa Mungu ni ishara ipi ya nyakati ipo katika vituko hivyo vya kusikitisha anavyovishuhudia vya kukataliwa ujumbe wake. Baada ya kuona uhalisia huo wa mambo anasali: “Nakushukuru Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako” (Mt 11:25).


Yesu anaanza kwa kumshukuru Baba yake. Kushukuru maana yake ni kutambua, kukiri, kusifu, kuungama kwa furaha mwanga, ufahamu na utambuzi alioweza kuupata kwa kuonana na Baba. Kwamba sasa ametambua sababu za kukataliwa kwake au sababu za mgomo na za watu kumshiti, licha ya harakati na kazi yote aliyofanya katika kutafuta kuwashirikisha watu mwenendo wa maisha. Hivi ndivyo anavyoingia katika majadiliano na Mungu ili kupata mwanga wake zaidi.

Katika injili unalikuta neno hili “Baba” yaani jinsi ya kumwita Mungu linajitokea mara 182. Aidha neno hili linatamkwa na Yesu tu, na kwa mara moja lilitamkwa na Filipo anapomwomba Yesu: “Bwana utuoneshe Baba yatutosha” (Yoh 14:8). Kumbe, mara nyingi Yesu anaposali analitumia jina hili Baba, au Abba, Dady, “Tata”! Katika fasuli ya Injili ya leo, unalisikia neno hili “Baba” linatamkwa mara tano likionesha mahusiano ya karibu sana na ya umwandani kati yake na Mungu. Marabi wa Kiyahudi hawakulitumia wanalitumia jina hilo, kwa sababu siyo neno la kiutu uzima na lenye hadhi, bali ni la kitoto, yaani ni jina la kimapendo linalotumika na mtoto katika kumwita baba yake ampendaye sana, Dady!

Kumbe Yesu ametaka tulitumie jina hilo kumwita Mungu, kwa vile Mungu wetu siyo wa kutisha, bali Mungu ni mapendo, anayetupenda na kutusaidia kama watoto wake wapendwa. Hivi hapa Yesu anatujulisha mahusiano ya upendo aliyo nayo yeye na Baba yake. Anatualika sisi tuwe na mahusiano hayo hayo na Mungu kama ya mtoto mdogo kwa baba yake mpendwa. Yesu anatambua kwamba huyu Mungu ndiye anayeongoza ulimwengu kwa namna ya pekee. Anataka tuelewe mantiki hii mpya ya mahusiano yetu na Mungu.


Kitu alichogundua Yesu katika sala ni kuwa mambo hayo yote aliyoyafanya Yesu, kumbe Mungu ameyafunua kwa watoto wadogo, “Mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga.” Huu ndiyo ukweli aliokuja kuugundua Yesu katika sala, kwamba Mungu ameufunua ukweli huo mkuu kwa watoto wadogo.

Kumbe ndugu zangu, wenye hekima na akili wanajiona wamekamilika, wameridhika na maisha yao, na maraharaha waliyo nayo. Mabadiliko na mambo hayo mapya ya Yesu Kristu yanawaletea vurugu. Wanajitosheleza, kama vile ilivyokuwa kule Nazareti alipojaribu kurudi mara moja, hawakumpokea tena, hata akawaambia: “Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani kwake” (Mark 6:4). Watu hao wenye hekima wanataka kushikilia mapokeo yao na hawataki mabadiliko ya mambo hata baada ya kuona ishara za mabadiliko ya nyakati. Hawa ndiyo wenye hekima hata kama hawajui kusoma na kuandika lakini wanajua yote.

Tunawapata watu namna hiyo katika maisha yetu, yaani watu wale wasiotaka kusoma, kutafakari biblia na kuona mabadiliko yaliyoko katika biblia. Watu wasioweza kusoma ishara za nyakati, hao ndiyo wanaojifanya mafundi wa kumkashifu Kristu. Huo ni mwaliko kwetu wa kuwavumilia na kuwaheshimu watu wa aina hii. Aidha huo ni mwito hata kwa viongozi wa kila aina, wakiwepo wale wa serikali, wa siasa na wa dini zozote zile, hususani kwa wazazi wanaotoa nguvu zao zote kusoma ishara za nyakati na kuwafundisha au kuwaonesha watoto wao uupya wa maisha. Lakini wao hawaelewi au wanaziba masikio yao.


Hao watoto wadogo anaowatamka Yesu, haina maana ya wale wasiojua, bali ni wale wasiojitoshelesha na wanaojua kwamba wakitaka furaha ya kweli wapokee fikra za Bwana wa Nazareti. Ujumbe wa Yesu na ufunuo wake ni zile heri nane. Alichokitegemea Yesu ni kuwa wataalamu na wenye hekima ndiyo wangezielewa na kuzipokea hizo heri nane na kuzifanyia kazi. Kumbe kinyume chake wao walizibeza. Kumbe sasa Yesu anatambua kuwa hayo ndiyo mambo yaliyokuwa katika mipango ya Mungu.


Mara nyingi tunalalamika, tunataka mambo yaende kama tunavyotaka sisi. Yesu anatualika kuangalia mambo kwa namna alivyofanya Yeye. Tuangalie mambo na kuishi maisha kwa utulivu na kumtegemea Mungu hasa mambo yanapotuendea kombo. Aidha, Yesu anatualika kuwapokea watu jinsi walivyo hata kama watu hao hawapokea mwito wa Mungu, tuone mambo vizuri, tuishi kwa utulivu. Yesu anatambua kwamba kukosekana kwa roho hiyo kunaweza kutusababishia kukata tamaa.


Yesu anaendelea na sala: “Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na yeyote ambaye Mwana apenda kumfunulia.” Huo ni mwito wa kuingia kwenye umoja na shukrani hii kwa Baba, inavyooneshwa na Yesu katika uchaguzi tunaotakiwa kuufanya. Kisha Yesu anatualika anasema: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.” Wanaalikwa kupumzika kwa sababu wamekabiliwa wamebebeshwa na mizigo mizito.

Ni wale waliokuwa wameshinikizwa na mafundisho ya wale wanaojidai kuwa ni wenye hekima na akili, waliochukua hadhi ya kuwa mababa wa kiroho, wamechukua hadhi ya Mungu, wanajidai kuwa ni miungu na wenye kutunga na kufuata sheria nyingi. Yesu anawaalika hao watoto wadogo kubeba mzigo wake ambao ni mwepesi.

Kwa kawaida mzigo huo ni yale magogo yanayofungwa kwenye shingo au mabega ya ngombe na kufungiwa mzigo. Mara nyingi hubebwa na ng’ombe wawili. Maana yake sasa nira hiyo itabebwa na wawili, yaani Yesu Kristu pamoja na kila mmoja wetu. Mzigo huo siyo mzito bali ni mwepesi kwa sababu unatokana na hadhi tuliyo nayo ndani yetu, yaani inatudai tuwe wenyewe, tujipokee jinsi tulivyo kwani tunabeba pamoja na Yesu.

Nira hiyo ni unyenyekevu ambao Yesu anatualika tuungane naye aliye mpole na mnyenyekevu. “Njoni kwangu mimi niliye mpole na mnyenyekevu wa moyo.” Wale walio tayari daima kujipokea na kusema: “haya ndiyo maisha”. Hali na mtazamo wa kutoa maisha kwa ajili ya ndugu. Hali ya kupenda kutokana na hali ya ndani ya Kristu iliyo ndani yetu. Ukipokea ndani mwako unyenyekevu wa Yesu, utaweza kujitenga pembeni na kujitazama katika kikoo cha Mungu kwa sala, na utafanikiwa kusoma kwa unyenyekevu ishara zote za nyakati na kuzipokea, na hatimaye hutakata tamaa bali utasali daima kama Kristu: “Nakushukuru Baba”.

Padre Alcuin Nyirenda, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.