2014-07-04 14:47:06

Jubilee ya miaka 500 tangu alipozaliwa Mtakatifu Theresa wa Avila


Baba Mtakatifu Francisko ameridhia kwa Majimbo yote Katoliki nchini Hispania kuadhimisha Mwaka wa Jubilee ya miaka mia tano tangu alipozaliwa Mtakatifu Theresa wa Avila, maadhimisho ambayo yataanza kutimua vumbi tarehe 15 Oktoba 2014 na kuhitimishwa rasmi hapo tarehe 15 Oktoba 2015.

Katika maadhimisho haya, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania amepewa kibali cha kutoa rehema na baraka za kipapa kwa waamini wote watakaoshiriki katika maadhimisho haya kwa kuzingatia masharti yaliyowekwa na Mama Kanisa ili kumwezesha mwamini kupata rehema kamili. Kwa waamini wanaotaka kupata rehema kamili, itawabidi kushiriki Ibada ya Misa Takatifu, kuungama, kupokea Ekaristi Takatifu na kusali kwa ajili ya nia ya nia za Baba Mtakatifu.

Mtakatifu Theresa wa Avila anayejulikana kama Theresa wa Yesu alizaliwa kunako tarehe 28 Machi 1515 huko Avilla, Hispania. Akiwa na umri wa miaka ishirini, alijiunga na Shirika la Watawa wa Karmeli, baada ya tafakari na hija ya maisha ya ndani aliyoifanya kwa kipindi cha miaka thelathini na tisa, aliweza kufikia wongofu wa ndani, akawa ni kati watu mashuhuri kabisa ndani ya Kanisa waliojikita katika mchakato wa mabadiliko ndani ya Kanisa, kwa maandiko lakini zaidi kwa njia ya ushuhuda wake wa maisha.

Mtakatifu Theresa wa Avilla akawa ni chachu ya maisha ya kitawa sehemu mbali mbali nchini Hispania. Akafariki dunia tarehe 15 Oktoba 1582. Akatangazwa kuwa Mwenyeheri na Papa Paulo V kunako mwaka 1614. Papa Gregorio XV kunako mwaka 1622 akamtangaza kuwa Mtakatifu. Mtumishi wa Mungu Papa Paulo VI kunako mwaka 1970 akamtangaza na kumwandika katika Orodha ya Walimu wa Kanisa Katoliki pamoja na Mtakatifu Katarina wa Sienna.








All the contents on this site are copyrighted ©.