2014-07-03 08:54:37

Je, upatanisho unawezekana Nigeria?


Kardinali John Onaiyekan Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria anasema, watu wamechoshwa na mashambulizi ya kigaidi yanayofanywa na Kikundi cha Boko Haram; wananchi na watu wenye mapenzi mema wanataka amani na utulivu, mambo msingi katika kukuza na kudumisha maendeleo ya watu kiroho na kimwili. RealAudioMP3

Wananchi wanataka kuona kwamba, uhuru wa kuabudu unaheshimiwa na kuthaminiwa na wote na kwamba, haki inashika mkondo wake bila kigugumizi chochote.

Kardinali Onaiyekan anasema, ikiwa kama kweli Boko Haram wanataka amani na upatanisho; wanataka kusitisha mashambulizi na nyanyaso na utekaji wa watu wasiokuwa na hatia, basi kuna haja ya kuanzisha mchakato wa majadiliano yanazozingatia ukweli na wote wanaoendelea kusababisha mashambulizi kwa watu wasiokuwa na hatia.

Inawezekana kabisa hata katika hali kama hii ambayo inaonesha kwamba watu wengi wamekata tamaa na wangependa kulipiza kisasi kwa kuhakikisha kwamba, Kikundi cha Boko Haram kinaoneshwa cha mtema kuni, lakini ukweli, upatanisho wa kitaifa na msamaha ni mambo yanayowezekana, ili Nigeria iweze kujikita tena katika amani na upatanisho, kwani chuki na dhana ya kulipizana kisasi itaendeleza machafuko na kinzani nchini humo pasi na suluhu ya kweli.

Serikali ya Nigeria na vyombo vya usalama wa taifa zimewekeza rasilimali watu na fedha kwa ajili ya kupambana na kikundi cha kigaidi cha Boko Haram, lakini matokeo yake ni watu bado wanaendelea kutekwa nyara, kuuwawa kikatili na kuchomewa nyumba zao. Msamaha unaweza kutolewa kwa wale ambao watakana na wala hawatajihusisha tena na vitendo vya kigaidi, ili kuanza maisha mapya.

Boko Haram wanapokamatwa, wanashitakiwa na kuhukumiwa kifo, matokeo yake ni kuongeza chuki na uhasama kati ya watu wasiokuwa na hatia. Hali kama hii ikiendelea hivi, hakuna uwezekano wa Kikundi cha Boko Haram kujisalimisha na hivyo kuanza mchakato wa ujenzi wa misingi ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa. Chuki, vita na uhasama ni cheche ambazo zitaendelea kuwavuruga wananchi wa Nigeria.

Kwa watu wanaotaka kuanza mchakato wa majadiliano ni alama wazi kuwa wanataka kuleta walau ufumbuzi wa tatizo ambalo linaendelea kusumbua vichwa vya watu wengi ndani na nje ya Nigeria. Kwa wale wanaotaka kugeuza maisha yao kwa kuachana na vitendo vya kigaidi, watendewe kwa haki na kwamba, watu walioathirika kwa vitendo vya kigaidi walipwe fidia!

Wazo kama hili la kufanya majadiliano na Kikundi cha Boko Haram liliwahi kujitokeza na Serikali ya Nigeria ikaonekana kana kwamba, imekunwa kidogo na wazo hili na kutaka kuridhia, lakini baada ya kushutumiwa na Jumuiya ya Kimataifa kwamba, Nigeria inajadiliana na Magaidi, ikabadili msimamo wake na kusema kwamba, Serikali ya Nigeria itakula sahani moja na magaidi, hadi pale kitakapoeleweka! Hapa ni falsafa ya jino kwa jicho inayotawala!








All the contents on this site are copyrighted ©.