2014-07-02 08:44:36

Ni majonzi tupu!


Kardinali Antonio Maria Vegliò, Rais wa Baraza la Kipapa la wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum anasema kwamba, kuna watu wanaendelea kufa maji katika Bahari ya Mediterrania, wakiwa na tumaini la kupata maisha bora ugenini. RealAudioMP3

Bara la Ulaya ni tumaini la wahamiaji wengi wanaoendelea kuhatarisha maisha yao kwa kukabiliana na hali ngumu jangwani na baharini, wachache wanafaulu kutua nanga ya matumaini, lakini kuna maelfu ya watu ambao wamepoteza maisha yao Jangwani na Baharini, wakiwa kwenye harakati za kuelekea Ulaya. Ni watu wanaozikwa kwenye makaburi yasiyokuwa na Misalaba chini ya Bahari.

Mitumbwi na mashua wanazotumia badala ya kuwapatia matumaini mapya ya maisha anasema Kardinali Vegliò imekuwa ni majeneza ya kuwasindikiza kwenye kina cha bahari. Hivi ndivyo alivyosema Baba Mtakatifu Francisko alipotembelea kwa mara ya kwanza Lampedusa hapo tarehe 7 Julai 2013, ili kushuhudia kwa macho yake mwenyewe mateso na mahangaiko ya wahamiaji, ambao wanaendelea kuweka rehani maisha yao wakiwa na matumaini ya kupata maisha bora zaidi.

Hawa ni watu wanaokimbia vita, nyanyaso na madhulumu; ni watu ambao wameonja adha ya maisha kutokana na umaskini wa hali na kipato; ni kundi la watu waliokata tamaa kutokana na kinzani za kidini, kijamii na kisiasa, kiasi kwamba, kwao maisha hayana thamani tena, hata kama watazama maji na kupotelea tumboni mwa bahari kwao si jambo la kuhuzunisha tena!

Hata pale wachache wanapofanikiwa kutua nanga ya matumaini kwa kufika Barani Ulaya, wanakumbana na sheria kali na baguzi, zinazowatenga na kuwanyanyasa kana kwamba, hakuna sheria za Kimataifa zinazosimamia na kuratibu hali ya wakimbizi na wahamiaji duniani.

Watu wa Ulaya inaonekana wamechoka kusikia kila wakati maafa ya wahamiaji na wakimbizi wanaopoteza maisha yao huko Jangwani na Baharini, wanasahau kwamba, watu ambao wameokolewa maisha yao ni tumaini kwa familia na jamii inayohusika.

Kardinali Vegliò anasema kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kutafuta suluhu makini zinazolinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu. Kwa wahamiaji wanaotafuta hifadhi ya kisiasa wasipewe mgongo, wasaidiwe kulingana na sheria na kanuni za kitaifa na kimataifa.

Kardinali Vegliò anawataka wakimbizi na wahamiaji wasithubutu kuhatarisha maisha yao kwa kujikabidhi mikononi mwa watu ambao wanauchu wa mali na utajiri wa haraka wanaowaahidia fanaka na maisha yenye raha ughaibuni, lakini wanasahau kwamba, wanawadanganya na kuwalaghai na wala ukweli haumo ndani mwao. Hii ni safari inayofanywa hata na watoto wadogo na wanawake wanaotembea na kifo miguuni pao!

Ni watu wasiokuwa na matumaini kwani mara nyingi watu kama hawa wanatumbukia katika mikono ya wafanyabiashara haramu ya binadamu au watu wanaojihusisha na utumwa mamboleo, kiasi kwamba, watu hawa wanaendelea kuteseka kiroho na kimwili na kwamba, utu na heshima yao havina thamani tena.

Kardinali Antonio Maria Vegliò, katika Ibada kwa ajili ya kuwaombea wahamiaji na wageni wanaokufa maji wakiwa njiani kwenda Barani Ulaya iliyofanyika hivi karibuni kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria wa Trastevere mjini Roma, anasema kwamba, kuna haja kweli ya kujenga na kudumisha utamaduni wa ukarimu kwa nchi za Ulaya, ili kweli Bahari ya Mediterrania iwe ni kielelezo cha matumaini, amani, upendo na mshikamano! Mahali ambapo watu wanaweza kusikia tena wakisalimiana, amani kwako, shallom, salam alay kum, pax vobiscum!

Imehaririwa na
Padre Richard a. Mjigwa, C.Pp.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.