Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni amefanyiwa mahojiano na Franca Giansoldati
wa Gazeti linalochapishwa kila siku mjini Roma, lijulikanalo kama Il Messaggero kwa
kusema kwamba, dhamana ya kimaadili inahitaji ujasiri na moyo mkuu.
Kwa ufupi
ni kiini cha majibu ambayo Baba Mtakatifu ameyatoa alipokuwa akijibu maswali mbali
mbali kuhusiana na changamoto zinazoikumba miji mikuu kama vile Roma; mabadiliko yanayodhohofisha
sera na mikakati ya kiuchumi; umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea mafao
ya wengi; maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; utu na heshima ya binadamu;
utumwa mamboleo unaowatmbukiza hata watoto katika biashara ya ngono; kazi za suluba
wanazofanyishwa watoto wadogo, kiasi cha kuathiri makuzi yao bila kusahau nyanyaso
za kijinsia dhidi ya watoto wadogo zinazofanywa na watu ambao wamepewa dhamana ya
kuwalinda na kuwasimamia watoto wadogo.
Baba Mtakatifu Francisko anakiri kwamba,
yeye ni mgeni sana mjini Roma kuna mambo mengi ambayo anaendelea kujifunza kwa mfano
tangu azaliwe hakuwahi kuingia kwenye Kikanisa cha Sistina kilichoko mjini Vatican,
eneo ambalo lina mvuto mkubwa kwa watalii kutoka sehemu mbali mbali za dunia, lakini
yeye ameingia humo kwa mara ya kwanza wakati wa uchaguzi wa Papa Benedikto XVI kunako
mwaka 2005 na kwamba, hajawahi kutembelea kwenye Makumbusho ya Vatican yenye utajiri
mkubwa wa sanaa kutoka sehemu mbali mbali za dunia.
Analifahamu sana Kanisa
la Bikira Maria mkuu kwani hapo mara nyingi alikwenda kusali. Amewahi kutoa huduma
za kichungaji wakati alipokuwa Kardinali kwenye Kanisa la Mtakatifu Laurent. Anakiri
kwamba, Piazza Navona anaifahamu kwani hapo kulikuwa na nyumba ya wageni aliyokuwa
anaitumia kila wakati alipokuwa anafika Roma.
Katika miji mikuu anawakumbuka
zaidi vijana na changamoto wanazokabiliana nazo mijini, ndiyo maana Mwezi Novemba
2014, kutafanyika Kongamano la shughuli za kichungaji kwenye miji mikuu litakaloadhimishwa
Jimbo kuu la Barcellona. Miji mikuu inafumbata tamaduni za watu mbali mbali, lakini
pia ina changamoto zake kwani huko kuna idadi kubwa ya wahamiaji na wageni wanaotafura
ubora na usalama wa maisha. Kanisa halina budi kusoma alama za nyakati ili kuwasaidia
wananchi wanaoishi mjini, ili waweze kuonja Injili ya Furaha.
Baba Mtakatifu
Francisko ni kati ya Mababa Watakatifu ambaye hakushiriki katika maadhimisho ya Mtaguso
mkuu wa Pili wa Vatican, lakini anatambua mchango mkubwa uliotolewa na Mtumishi wa
Mungu Papa Paulo VI katika mchakato wa Uinjilishaji. Waraka wake wa Evangelii Nuntiandi
ni dira na mwongozo kwa Kanisa katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya.
Kwa watumishi
wa Serikali, wanapaswa kwanza kabisa kusimama kidete kulinda na kutetea mafao ya wengi,
utu na heshima ya binadamu, zawadi ya maisha tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni
mwa mama yake hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu na kwamba,
mwanasiasa anapaswa kujikita katika fadhila ya upendo. Tatizo kubwa linalojitokeza
katika siasa ni: rushwa, ufisadi na wizi wa mali ya umma.
Huduma kwa wananchi
inapaswa kuwa ni msingi bora kwa wale wote wanaotaka kupewa fursa za kuongoza wananchi
katika mchakato wa kujiletea maendeleo endelevu. Matatizo haya ya kijamii yamepembuliwa
vyema sana katika Liturujia ya Neno la Mungu kwa siku za hivi karibuni na kwamba,
amepata nafasi ya kuwashirikisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kile kilichomgusa
katika Neno la Mungu.
Anasema mla rushwa na mpenda rushwa hana rafiki. Rushwa
na ufisadi kwa sasa ni majanga ya kimataifa. Wanasiasa wengi waliofanya mabadiliko
wamepelekea wakati mwingine kumong’onyoka kwa tunu msingi za kimaadili katika masuala
ya kisiasa, kiuchumi na katika vyombo vya fedha. Mtikisiko wa uchumi kimataifa ni
matunda ya ubinafsi na rushwa!
Baba Mtakatifu anasema, anasikitishwa sana
na umaskini wa hali na kipato na anakwazika zaidi na mmon’gonyoko wa maadili na utu
wema; kwani haya ni mambo ambayo yanagusa utu na heshima ya binadamu. Biashara ya
utumwa mamboleo; biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya ni mambo yanayowaathiri
vijana, lakini yanachochewa na watu wazima wenye uchu wa mali na utajiri wa haraka
haraka, watu waliofilisika kimaadili na kiutu. Sera makini za kijamii zinaweza kusaidia
kukuza na kuboresha maadili na utu wema.
Kanisa halina budi kujielekeza zaidi
na zaidi katika kuwajengea watu uwezo wa kupambana na changamoto za maisha kwa kukuza
na kudumisha dhamiri nyofu. Waamini wapewe majiundo awali na endelevu kuhusu: Kanuni
ya Imani, Sakramenti za Kanisa, Maisha adili na maisha ya Sala, kwa ufupi waamini
wajitahidi kuifahamu Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, ili kuimwilisha katika uhalisia
wa maisha!
Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema
kukumbatia Injili ya Uhai na kuachana kabisa na utamaduni wa kifo unaokumbatia sera
za utoaji mimba. Watoto ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu wapokelewe na kutunzwa
kwa heshima zote. Watu wasiwe ni watuma wa mali, madaraka na sifa. Mafundisho ya Heri
za Mlimani ni muhtasari wa kanuni msingi za maisha ya Kikristo. Wanawake wanayo nafasi
kubwa katika maisha na utume wa Kanisa, kwani Kanisa linajitambulisha kuwa ni Mama
na Mwalimu.
Baba Mtakatifu anasema, katika mikakati yake ya shughuli za kichungaji
kwa sasa anapenda kujielekeza zaidi Barani Asia. Mwezi Agosti anatarajiwa kushiriki
katika Kongamano la sita la Vijana wa Bara la Asia litakaloadhimishwa huko Korea ya
Kusini.
Mwezi Januari anatarajiwa kwenda nchini Sri Lanka na Ufilippini, kwa
hakika kuna matumaini makubwa kwa Kanisa Barani Asia. Nchini Korea, Kanisa linategemezwa
na waamini walei, matendo makuu ya Mungu. Hapa kuna waamini ambao wamejisaka kwa ajili
ya Kristo na Kanisa lake. China bado ni changamoto kubwa katika maisha na utume wa
Kanisa.
Baba Mtakatifu Francisko anasema kwa sasa anatekeleza changamoto na
maelekezo yaliyotolewa na Makardinali katika mikutano yao elekezi wakati wa uchaguzi
wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Hana jipya analolifanya, bali ni mwendelezo wa maisha
na utume wake hata kabla ya kuchaguliwa kuliongoza Kanisa. Hakuna jambo ambalo analifanya
katika upweke, haya ni matunda ya uongozi shirikishi ndani ya Kanisa, kwa kukazia
umuhimu wa Sinodi, ingawa ni dhana ambayo Makardinali wengi hawapendi kuisikia.
Mwishoni,
Baba Mtakatifu anawashukuru waamini wa Jimbo kuu la Roma katika Maadhimisho ya Sherehe
ya Watakatifu Petro na Paul, waendelee kuonesha ujasiri na ushuhuda wa imani, daima
wakiwa na furaha, matumaini na imani inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake,
licha ya magumu na changamoto wanazokabiliana nazo katika maisha kwa wakati huu!
Mahojiano
haya yamehaririwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio
Vatican.