2014-07-01 11:02:24

Dumisheni umoja!


Mara baada ya Maadhimisho ya Siku kuu ya Watakatifu Petro na Paulo iliyoadhimishwa mjini Vatican na Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili tarehe 29 Juni 2014 na kuwavika Maaskofu wakuu Palio Takatifu, Watanzania wanaosoma na kuishi mjini Roma walikusanyika kwa hafla fupi, ili kumpongeza Askofu mkuu Damian Denis Dallu wa Jimbo kuu la Songea.

Katika nasaha zake kwa watanzania, Askofu mkuu Dallu amewataka watanzania kuombea umoja wa nafsi unaojengwa katika upendo unaobubujika kutoka kwa Yesu Kristo; umoja wa taifa la Tanzania unaopaswa kujengeka kutokana umoja wa nafsi, ili Tanzania iweze kuendelea kuwa ni taifa linalojengeka kutokana na umoja wa nafsi na wala si vinginevyo; taifa linalojikita katika umoja wa kitaifa kwa kukazia misingi mikuu inayowaunganisha watanzania licha ya tofauti zao za kisiasa, kidini na kikabila.

Askofu mkuu Dallu amewataka watanzania kutokubali kumegwa wala kugawinyika kwa misingi yoyote ile kwani makundi ya namna hii yanaweza kukosa mwelekeo na dira katika ujenzi wa misingi ya umoja wa kitaifa inayojika katika ukweli, upendo, haki na amani.

Naye Padri Dietrich Canisius Pendawazima Kihaule, Makamu mkuu wa Shirika la Wamissionari wa Consolata katika mahojiano maalum na Radio Vatican anasema ameguswa sana na ujumbe uliotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa mahubiri yake, kwa kuwataka Maaskofu na waamini wote kutokuwa na woga wa kuhubiri Injili, Kumtangaza na Kumshuhudia Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.

Anasema, Yesu anawapatia wafuasi wake nguvu na ujasiri wa kushinda woga na wasi wasi, ili kusonga mbele kwa ujasiri na matumaini makubwa, kwa kutangaza na kuumwilisha upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Anawahimiza waamini kuwa imara na hodari ili kumshuhudia Kristo katika maisha ya kila siku!







All the contents on this site are copyrighted ©.