Askofu mkuu Damian Dallu wa Jimbo kuu la Songea, Tanzania ni kati ya Maaskofu wakuu
27 waliovikwa Pallio Takatifu wakati wa maadhimisho ya Siku kuu ya Watakatifu Petro
na Paulo, mitume, katika Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko
kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 29 Juni 2014.
Katika mahojiano
maalum na Radio Vatican, Askofu mkuu Dallu anamshukuru Mwenyezi Mungu, Baba Mtakatifu
Francisko, Kanisa la Tanzania na kwa namna ya pekee Jimbo kuu la Songea. Anasema amepata
fursa ya kuiombea Familia ya Mungu katika ujumla wake wakati wa maadhimisho ya Siku
kuu ya Wakatifu Petro na Paulo mitume na kwamba, anamshukuru Mungu kwa wema na baraka
zake anazolikirimia Kanisa.
Anasema, kwa maombezi ya Watakatifu Petro na Paulo
Mitume, waamini wajitahidi kuwa kweli ni mashahidi wa imani, kwa kujitoa bila ya kujibakiza.
Ametumia fursa hii pia kuliombea Taifa la Tanzania ili liweze kuendelea kustawi katika
upendo, umoja na mshikamano wa kitaifa kwa ajili ya kumtukuza Mungu, ili kwamba, umoja
na mshikamano miongoni mwa watanzania uweze kuzaa matunda ya umoja wa mataifa yote.
Naye
Padre Alcuin Nyirenda, OSB katika mahojiano na Radio Vatican amegusia historia fupi
ya Pallio Takatifu wanayovishwa Maaskofu wakuu kama alama ya mshikamano na Khalifa
wa Mtakatifu Petro, changamoto na mwaliko kwa Maaskofu wakuu kuwa kweli ni Wachungaji
wema wanaoweza kuthubutu kujisadaka kwa ajili ya kuwatafuta Kondoo waliopotea. Kwa
mara ya kwanza katika historia ya Kanisa, Pallio Takatifu ilitolewa na Papa Gregory
Mkuu alipomtuma Askofu mkuu Augustino wa Cantebury kwenda Uingereza kwa ajili ya kuinjilisha.
Ni
katika mantiki hii kwamba, Askofu mkuu Damian Dennis Dallu wa Jimbo kuu la Songea
kama mmissionari anatumwa na Mama Kanisa kuwaitangazia Familia ya Mungu Jimbo kuu
la Songea Injili ya Furaha na Matumaini. Anatumwa kutangaza na kulishuhudia Neno la
Mungu, ili kweli Kanisa Katoliki Jimbo kuu la Songea, liweze kujipambanua kuwa ni
Kanisa la Kristo linalosimikwa katika misingi ya umoja, upendo na mshikamano kama
Jumuiya ya Waamini.