Bado kuna watu wanamwaga damu yao kama ushuhuda kwa Kristo na Kanisa lake!
Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 30 Juni 2013 katika mahubiri yake kwenye
Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican, wakati Mama Kanisa anaadhimisha
Kumbu kumbu ya Wafiadini wa kwanza wa Roma anasema kwamba, leo hii kuna wafiadini
wengi zaidi kuliko hata ilivyokuwa kwenye Kanisa la Mwanzo.
Damu ya mashahidi
hawa imekua ni mbegu ya Ukristo kwa Roma na viunga vyake. Hii ni kazi kubwa inayofanywa
na Mwenyezi Mungu na kwamba, kukua na kushamiri kwa Kanisa ni matunda ya kazi ya Roho
Mtakatifu anayewawezesha Wakristo kushuhudia imani yao katika matendo! Mashahidi ni
watu ambao wamejisadaka kwa ajili ya kuonesha ile nguvu ya Injili iliyoko ndani mwao.
Ni watu ambao wamelirutubisha Kanisa kwa njia ya damu yao, lakini waamini wanakumbushwa
kwamba, ushuhuda kwa Kristo na Kanisa lake unapaswa kutolewa na waamini katika hija
ya maisha yao ya kila na siku na kilele chake ni pale wanapojisadaka kwa kumwaga damu
yao kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.
Ushuhuda huu unapaswa kujionesha katika
mtu ambaye amejizatiti barabara kumfuasa Kristo pasi ya kubadili msimamo na mawazo
yake, kwa kujikita katika uhuru na ukweli na kwamba, huu ndio ushuhuda unaotakiwa
na Yesu. Kanisa limekuwa na kukomaa mjini Roma, lakini bado kuna watu wanaoendelea
kuteswa na kudhulumiwa sehemu mbali mbali za dunia. Hali si shwari sana huko Mashariki
ya Kati.