Sanaa ni sehemu ya mchakato wa majadiliano ya Kiekumene
Katika mkesha wa Sherehe ya Watakatifu Petro na Paulo, Jumamosi tarehe 28 Juni 2014,
Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican pamoja na viongozi mbali mbali wa
Kanisa na Serikali wameshiriki katika tamasha la nyimbo za dini lililoongozwa na Kwaya
kutoka Upatriaki wa Mosco na kwaya ya Kikanisa cha Sistina, kama sehemu ya mchakato
wa kukoleza majadiliano ya kiekumene kwa njia ya nyimbo. Kwaya hizi mbili pia zimeshirikiana
kwa pamoja katika Ibada ya Sherehe ya Watakatifu Petro na Paulo kwenye Kanisa kuu
la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 29 Juni 2014.
Kardinali
Parolin amewashukuru wafadhili na wadau mbali mbali kwa kuwezesha kwaya hizi mashuhuri
kutumbuiza na kwa namna ya pekee, ametoa shukrani zake za dhati kwa Patriaki Kirill
na kwa Kanisa zima la Kiorthodox la Moscow, kwa kufanikisha tukio hili ambalo ni mwendelezo
wa hija ya pamoja kati ya Kanisa la Kiorthodox na Kanisa Katoliki, ili kushirikishana
uzoefu na mang'amuzi kwa kulenga umoja kamili kati ya Wakristo.
Kuna uhusiano
wa karibu sana na Fumbo la Mungu kwa wale wanaotafuta kilicho kweli, chema na kitakatifu.
Kwa wasanii wa Kikristo wanaojisadaka kwa kusukumwa na imani watambue kwamba, wanatekeleza
utume wao wa Kikanisa kwa ajili ya huduma kwa utukufu wa Mungu na mng'ao wa sura ya
Kristo. Kuna tofauti kubwa ya mapokeo ya muziki mtakatifu kati ya Kwaya hizi mbili,
lakini zote kwa pamoja zimewawezesha kuonjesha uzuri wa kukutana mbele ya Mkombozi.
Kardinali
Parorin anasema, sanaa pia inapaswa kuwa ni sehemu ya mchakato wa majadiliano ya kiekumene
kati ya Makanisa ya Mashariki na Makanisa ya Magharibi, ili kwa pamoja waweze kuchangia
utajiri huu kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu, kwa kukuza na kutukuza kazi ya
uumbaji, madhara ya dhambi sanjari na ukombozi wa mwanadamu.
Muziki mtakatifu
unafumbatwa pia katika Fumbo la neema ya Mungu inayowahamasisha Wakristo kutafuta
umoja kamili. Ushiriki wa kwaya hizi mbili katika Ibada ya Misa Takatifu katika maadhimisho
ya Sherehe ya Watakatifu Petro na Paulo miamba wa imani ni kielelezo makini cha ile
hamu ya umoja na mshikamano miongoni mwa Wakristo. Hii ni kiu ya kutaka kutembea kwa
pamoja, kwa kushirikiana kwa ajili ya mafao ya wengi na kwamba, waendelee kusali kwa
ajili ya kuombea umoja wa Kanisa kadiri ya mapenzi ya Kristo mwenyewe.